Tuesday 19 November 2013

Nape apendekeza Msajili wa vyama kufuta Chadema


Na Joyce Joliga, Mwananchi

Posted  Jumanne,Novemba19  2013  saa 24:0 AM
Kwa ufupi
Nape licha ya kukiandama Chadama alisikitika hakuna waziri wa kilimo aliyewahi kwenda mkoani Ruvuma.

Songea. Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nauye amemtaka Msajili wa Vyama vya Siasa nchini kukifuta Chadema kwa madai kuwa, kimeshindwa kusimamia katiba yake kwa kutofanya uchaguzi wa ndani zaidi ya miaka zaidi ya kumi.

Nape alisema chama hicho kimejaa viongozi waongo, wapenda vurugu na wanaotaka kuvuruga amani ya nchi kwa kisingizio cha Katiba Mpya na kwamba, wamesahau katiba iliyopo imedumu kwa miaka 50 na haijawahi kuwagombanisha wananchi wala kuwavuruga.
Hata hivyo, jitihada za kumpata Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Chadema, John Mnyika kuzungumzia tuhuma hizo jana jioni kwa simu yake haikufanikiwa.
Akihutubia wakazi wa Manispaa ya Songea jana, Nape alimtaka Msajili wa Vyama vya Siasa kukiagiza chama hicho kufanya mkutano wa uchaguzi haraka kikigoma akifute na kwamba, asipofanya hivyo wao wataendelea kumsema na kumchukulia hatua.
Aliongeza CCM kilifanya uchaguzi wake 2012 na kupata viongozi wapya, lakini Chadema imeshindwa kusimamia katiba yake ambayo ilipeleka kwa msajili wa vyama na kuisajili kwa kuivunja wao wenyewe kwa kuendesha chama isivyo.
Nape alisema chama hicho hakifai kuongoza nchi, kwani kimeshindwa kusimamia katiba yake na kuifuata hakiwezi kuongoza wananchi.
“Kwa sababu Msajili wa Siasa ni mlezi wa vyama vyote vya siasa ikiwamo Chadema, namuomba akiagize chama hicho kifanye uchaguzi kwani wao wanajiita wanademokrasia wakati wanashindwa kufuata demokrasia kwa vitendo,” alisema Nape.
Kuhusu malalamiko ya wananchi, Nape alisema wananchi wamekuwa wakilalamikia utendaji mbovu wa viongozi wa Serikali na kwamba, yana msingi kwani inasikitisha licha ya Ruvuma kuwa ni mkoa unaolisha nchi, hakuna mawazili wa kilimo ambao wamefika mkoani hapa.

SOURCE: MWANANCHI