Thursday 14 November 2013

Hali ni Mbaya : Rais Museveni wa Uganda AMSALITI Rais Kagame wa Rwanda na kumpa ushauri ule ule uliomkosanisha na Rais Kikwete


WAKATI hatima ya kutiwa saini mkataba wa amani kati ya Serikali ya DRC na waasi waliosambaratishwa wa M23 ikiwa haijulikana, uhusiano wa maswahiba wawili wa eneo la Maziwa Makuu, Rais Yoweri Museveni wa Uganda na Paul Kagame wa Rwanda umetikisika baada ya Museveni kumtaka mwenzake huyo azungumze na waasi.

Ni ushauri kama huo aliopewa Kagame Mei mwaka huu na Rais Jakaya Kikwete ukilenga kuleta na kuimarisha amani Mashariki mwa Congo ndio ulioyumbisha uhusiano kati ya Tanzania na Rwanda, kabla ya Kikwete kuifafanua na kisha kukutana na Kagame jijini Kampala, Uganda Agosti mwaka huu.

 


Kwa mujibu wa mtandao wa AfroAmerica Network, Museveni, baada ya kurejea kutoka kwenye mkutano wa wakuu wa nchi za SADC na zile za Maziwa Makuu (IGGLR) huko Pretoria, Afrika Kusini wiki iliyopita, alimpigia simu Kagame na kumwambia: “Huenda sasa ni wakati muafaka wa kuzungumza na wapinzani wako wenye silaha.”

Chanzo cha habari cha mtandao huo kimemnukuu mmoja kati ya viongozi wa juu wa Jeshi la Rwanda (RDF), akisema Museveni alimwomba Kagame kuzungumza na waasi hao haraka kabla muda haujapita mara tu Rais huyo wa Uganda aliporejea Kampala Alhamisi iliyopita.

Mkutano wa pamoja wa wakuu wa nchi za SADC na ICGLR uliofanyika kuanzia Jumatatu wiki iliyopita chini ya uenyekiti wa marais watatu, Joyce Banda (Malawi, SADC), Museveni (Uganda, ICGLR) na wa Afrika Kusini, Jacob Zuma, ulitoa wito kwa M23 kuweka silaha chini. Siku mbili baadaye waasi hao wanaodaiwa kuungwa mkono na Rwanda, walishindwa vita na kutangaza kuacha uasi.

Kagame hakuhudhuria mkutano huo, badala yake aliwakilishwa na Waziri wa Mambo ya Nje, Louise Mushikiwabo.

“Ni ushauri tu. Nimerejea kutoka kwenye mkutano na SADC uliojadili amani eneo la Maziwa Makuu. Bahati mbaya inaonekana kwamba karibu viongozi wote wanaamini kikwazo kikubwa cha amani ni kuwapo kwa waasi wa Kinyarwanda mashariki mwa DRC.

“Hakika suala hili linapaswa kuzungumzwa kwa njia moja au nyingine. Na viongozi hao wanaamini kwamba hili halitatatuliwa bila serikali ya Rwanda kukaa kwenye meza ya usuluhishi na wapinzani wake wenye silaha. Hata mimi ninaamini hivyo, huenda wakati umefika kwako kuzungumza nao,” alinukuliwa Museveni akimwambia Kagame katika mazungumzo ya simu yaliyodumu kwa takriban dakika 15.

Kagame alijibu: “Sitozungumza na FDLR, washiriki wa mauaji ya kimbari. Never, … , ever. Sitozungumza kamwe na wahalifu.”

Hata hivyo, inadaiwa Museveni alimkumbusha Kagame kuwa si waasi wote wa Rwanda walioko DRC ni wanachama wa FDLR au wahalifu  na kwamba wapo anaoweza kuzungumza nao kwa kuanzia.

Baada ya mazungumzo hayo, Kagame aliitisha mkutano wa dharura na washauri wake wakuu na kuwaeleza walichozungumza na Museveni na kuongeza:

Nimekuwa nikiwaambia mara kwa mara kuwa tuko peke yetu. Hata Yoweri, tuliyemwamini kama rafiki yetu na mwenzetu anatugeuka! Leo anatuambia hiki, kesho anakwenda kukutana na viongozi wengine na kutubadilikia.

Baadaye akawataka washauri hao kuja na mpango mkakati wa nini cha kufanya wakati huu Rwanda ikizidi kutengwa na nchi za Afrika na hata za nje ya Afrika.

Mwanzoni mwa mwezi, Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, John Kerry na mwenzake wa Uingereza walimwonya Kagame kuachana mara moja na ushiriki wake kwenye machafuko ya mashariki mwa DRC, ikiwa ni mara ya pili ndani ya mwaka mmoja kwa wakubwa hao kutoa onyo kama hilo.

Wakati hayo yakiendelea, zipo taarifa kwamba Rais Museveni amepanga kutuma ujumbe nchini kuja kuzungumzia mustakabali wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) baada ya Rais Jakaya Kikwete kuwaambia Watanzania kwamba Tanzania haijakiuka chochote katika makubaliano ya msingi, ila wenzetu hao ndio huenda wana ajenda yao.

Kauli ya Kikwete ilihitimisha hali ya wasiwasi wa Tanzania kujitoa EAC na iwapo ujumbe wa Uganda utakuja, itakuwa ni mwendelezo wa kilichofanywa mwishoni mwa wiki na Kenya waliomtuma Waziri wa Mambo ya Nje kuja Dar es Salaam kuweka mambo sawa.


Mapema wiki hii, aliyekuwa Mwanasheria wa Serikali ya Kenya, Amos Wako ambaye pia ni Seneta wa Bisia alitoa wito kwa Rais Uhuru Kenyatta kuhakikisha kuwa EAC haisambaratiki, akidai kuwa watakaoumia zaidi ni Wakenya.

Wako aliyekuwa kwenye mkutano wa hadhara pamoja na Mbunge wa Budalangi, Ababu Namwumba, alisema wakati jumuiya ya awali ilipovunjika mwaka 1977, Wakenya wengi waliokuwa wakifanyakazi nje ya nchi ndio walioathirika zaidi.

“Wapo watu mashuhuri kama Raila Odinga na Kalonzo Musyoka wanaokubalika ndani na nje ya nchi ambao kama Uhuru anataka wanaweza kumsaidia kuzungumza na Rais Kikwete wa Tanzania. Hatutaki jumuiya hii ivunjike, si busara hata kidogo,” alisema Wako.

-Mtanzania