Wednesday 13 November 2013

Dk Shein: Mimi ndiye msemaji mkuu wa Z’bar


Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein akijibu maswali ya waandishi wa habari jana alipokutana nao Ikulu mjini Zanzibar. Picha na Martin Kabemba 
Na Rashid Kejo,Mwinyi Sadallah, Mwananchi

Posted  Jumatano,Novemba13  2013  saa 24:0 AM
Kwa ufupi
Azungumzia tathmini ya uongozi wake chini ya Serikali ya umoja wa kitaifa kwa miaka mitatu.


Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein amesema hakuna kiongozi yeyote wa Zanzibar mwenye mamlaka ya kuzungumzia msimamo wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) kuhusu masuala ya Katiba na Muungano isipokuwa yeye na kwamba kauli ambazo zimekuwa zikitolewa na Makamu wake wa Kwanza, Maalim Seif Sharif Hamad ni zake binafsi au za chama chake.
Akizungumza na waandishi wa habari Ikulu, Zanzibar jana juu ya tathmini ya uongozi wa Awamu ya Saba anayoiongoza, Dk Shein alisema kuna changamoto kubwa za kuendesha Serikali ya Umoja wa Kitaifa na kwamba jambo muhimu ni kuvumiliana.
Tangu kuanza kwa mchakato wa Katiba Mpya, msimamo wa Maalim Seif ambaye pia ni Katibu Mkuu wa CUF, umekuwa ni kuundwa kwa Serikali Tatu au ya Mkataba, ambao unapingana na ule wa CCM, wa kutaka Serikali mbili kama ilivyo sasa.
Rasimu ya kwanza iliyotolewa na Tume ya Marekebisho ya Sheria imependekeza kuwapo kwa Serikali Tatu, ya Muungano, Tanganyika na Zanzibar.
“Serikali yangu haina msimamo wa jambo hilo. Kila mwananchi ana uhuru wa kutoa maoni yake, ninaweza kutoa msimamo kutokana yaliofikiwa na uamuzi wa chama changu na kila mtu anaweza kufanya hivyo na si kuisemea Zanzibar na wananachi wake.”
Alimsifu Rais Jakaya Kikwete kwa dhamira yake ya kusimamia suala la mabadiliko ya Katiba na mchakato ulivyokwenda na sasa taifa linaelekea kupata Bunge la Katiba kabla ya kufanyika kwa kura ya maoni mwakani.
Akizungumzia Serikali ya Umoja wa Kitaifa, Dk Shein alisema imefanikiwa kudumu kwa miaka mitatu sasa kutokana na kuvumiliana na kufanya kazi kwa pamoja bila ya kutanguliza itikadi za kisiasa. “Nchi nyingi zimejaribu hili zimeshindwa, lakini sisi tumefanikiwa kwa sababu tunavumiliana. Hili linahitaji stahimili kubwa vinginevyo tutagawana mbao na sitaki hili litokee kwenye uongozi wangu.”
Akizungumzia masuala ya Muungano, Dk Shein alisema licha ya mchakato wa Katiba Mpya kuendelea, Serikali zote mbili (Muungano na Zanzibar), zimeendelea kujadili masuala muhimu na changamoto zilizopo na kusema siyo sahihi kubeza mgawo wa sasa wa mapato ya Muungano ambao Zanzibar inapata asilimia 4.5.
“Jeshi la Wananchi na JKT (Jeshi la Kujenga Taifa) wanatumia mabilioni mangapi, Mambo ya Nje, Mambo ya Ndani, Elimu ya Juu Sayansi na Teknolojia... Sisi (Zanzibar tunatoa ngapi?)”
Uchumi
Akizungumzia ukuaji wa uchumi katika kipindi cha miaka mitatu ya uongozi wake, Dk Shein alisema kumekuwa na ongezeko kubwa la ukusanyaji wa mapato akisema katika mwaka wa fedha wa 2010/11 Sh181.4 bilioni zilikusanywa na mwaka uliofuata wa 2011/12 makusanyo yaliongezeka hadi kufikia Sh212 bilioni na mwaka wa fedha wa 2012/13 kiasi hicho kimeongezeka hadi kufikia Sh266. 2 bilioni.
Alisema uchumi wa Zanzibar umekuwa ukiongezeka mwaka hadi mwaka. Alisema mwaka 2010 uchumi ulikua kwa asilimia 6.4, mwaka 2011 asilimia 6.7, mwaka 2012 asilimia saba na mwaka huu unatarajiwa kukua hadi kufikia asilimia 7.5.

SOMA ZAIDI HABARI HII: mwananchi