Thursday 14 November 2013

Aomba kuahirishwa adhabu ya kunyongwa ili amsaidie mama kupata viungo vyake


 14 Novemba, 2013 - Saa 12:47 GMT

Ronaldo Phillips mfungwa anayetarajiwa kunyongwa Marekani
Hukumu ya kunyongwa kwa Ronald Philllips aliyepatikana na hatia ya kumuua mtoto wa miaka mitatu katika jimbo la Ohio nchini Marekan imeahirishwa kutokana na mshitakiwa huyo kuomba kuchangia baadhi ya viungo vyake vya mwili zikiwemo figo ili kunusuru uhai wa mama anayeumwa.

Ronald Phillips alitarajiwa kunyongwa Alhamis kwa njia ya sindano ya sumu baada ya kupatiakana na hatia ya kumuua mtoto wa kike mwenye umri wa miaka mitatu mwaka 1993.

Gavana wa jimbo la Ohio John Kasich amesema kama ombi hilo la mshitakiwa litasaidia kuokoa uhai wa mtu mwingine basi na likubalike, lakini litakuwa jambo geni kuahirishwa kwa adhabu iliyokwisha kupitishwa japo kuwa madaktari wanapaswa kuthibitisha.

Phillips mwenye umri wa miaka 40 alihukumiwa kifo kutokana na makosa ya ubakaji na mauaji ya binti wa rafiki yake wa kike Sheila Marie Evans.

Dawa ya sumu iliyotarajiwa kutumika kumuua Phillips ni aina ya midazolam na hydromorphone, mchanganyiko wa dawa ambayo ingetumika kwa mara ya kwanza nchini Marekani kunyonga watu
Jimbo la Ohio liliamua kutumia mchanganyiko wa dawa hii kwa sababu haikuwa na kiasi cha kutosha cha dawa ya kawaida inayotumika kunyongea watu ijulikanayo kama pentobarbital.

Mama mzazi wa Phillips amekuwa akisumbuliwa na maradhi ya figo na dada yake Phillips pia anasumbuliwa na maradhi ya moyo ambapo anasema anahitaji kutoa viungo vyake haraka iwezekanavyo.

CHANZO: BBC SWAHILI