Tuesday 1 October 2013

WALIOSHITAKIWA KWA KUTAKA KUMUUA NYERERE MWAKA 1970

 

Mwalimu Julius Nyerere.
MUONGO wa kwanza tangu uhuru kulijitokeza mambo mengi  na mengine hayakujulikana kwa wengi  na huenda hayatajulikana hata sasa hasa kwa vijana wa leo.

Tukio muhimu zaidi lililotokea mwishoni mwa mwaka 1969 na mwanzoni mwa mwaka 1970 ni kuvurugwa kwa mpango wa kumuua na kuiangusha Serikali ya Julius Nyerere.
Oscar Kambona ambaye habari zake nimeziandika katika safu hii siku za nyuma alitajwatajwa kuhusika katika maasi hayo, lakini ni jambo lisilothibitishwa hadi leo.

Pamoja na Kambona ambaye wakati wa maasi hayo ya mara ya pili alikuwa uhamishoni Uingereza, walihusishwa watu wengine waliodaiwa kutaka kuiangusha serikali hiyo ya Mwalimu Nyerere.
Baada ya habari hizo kubumburuka watuhumiwa wengi walikamatwa na vyombo vya usalama vikiongozwa na idara ya usalama wa taifa na kufikishwa polisi kwa mahojiano.

Hata hivyo, kulikuwa na mchujo na wafuatao walifikishwa mahakamani.
 Kesi yao ilianza kunguruma Jumatatu ya Juni 8, 1970 katika Mahakama Kuu ya Tanzania mbele ya Jaji Mkuu, P. T. Georges.
Nchi nzima watu wakawa na wasiwasi kutokana na minong’ono kuwa kuna watu walitaka kumuua Nyerere na kisha kuipindua serikali yake.

Baada ya siku chache watuhumiwa wa jaribio hilo wakatangaza na kufikishwa mahakamani. Watu hao ni Gray Likungu Mattaka, John Dunstan Lifa Chipaka, Bibi Titi Mohamed, Michael Marshall Mowbray Kamaliza, Eliyah Dunstan Lifa Chipaka, William Makori Chacha na Alfred Philip Milinga.
Wote hao walijikuta wakifikishwa mahakamani kwa kosa la uhaini wakituhumiwa kula njama za kuiangusha Serikali ya Tanzania na kumuua Rais wake, Mwalimu Nyerere.

Gray Likungu Mattaka (34) ambaye awali alikuwa Mhariri wa Habari katika magazeti ya chama cha TANU, The Nationalist na Uhuru, ilielezwa mahakamani kuwa alijulikana pia kwa majina bandia ya ‘kazi’ ambayo ni Chaima, Kavuma, Mikaya au Edward Kavuma.

Naye John Dunstun Lifa Chipaka (38) alikuwa katibu wa zamani wa Chama cha Congress. Kwa mujibu wa hati za mashitaka, alikuwa na majina mengine ya bandia kama M. M. Chimwala, Chimwala Ching’wechene, Chimwala au Padre John Chimwala.

BIBI TITI ALIVYOPANGA KUMUUA NYERERE

Bibi Titi na Mwalimu wakihutubia wananchi enzi za TANU.
WIKI iliyopita niliandika juu ya kesi ya uhaini iliyoanza kunguruma Juni 8, 1970 katika Mahakama Kuu ya Tanzania, Dar.
Niliwataja pia baadhi ya watuhumiwa waliofikishwa mahakamani lakini mtuhumiwa mmoja alishangaza wengi na si mwingine isipokuwa ni Bibi Titi Mohammed (45).
Wengi walishangaa na kujiuliza, mama huyu kweli alitaka kumuua Rais Julius Nyerere? Walijiuliza hivyo kwa sababu enzi hizo mwanamke kujihusisha na kitu kizito kama hicho ilikuwa ni ndoto, lakini yeye alifanya na alimwaga fedha kwa kazi hiyo.

Lakini pia wananchi walishangaa kwa kuwa Bibi Titi aliwahi kuwa waziri na rais wa Umoja wa Wanawake wa Tanzania (UWT).

Kama ilivyo kwa watuhumiwa wengine ambao walikuwa na majina bandia ya ‘kazi’. Mama huyo naye mahakama iliambiwa alikuwa na majina mengine aliyojiita au kuitwa nayo ambayo ni Mama Mkuu, Mwamba au Anti wakati wa mipango yao ya mauaji na kuipindua serikali ya Nyerere.
Bibi Titi aliyezaliwa mwaka 1926 alikuwa kivutio kila alipokuwa anafikishwa mahakamani kwani wakati wa ujana wake alikuwa mtu wa karibu wa Nyerere.

Alishirikiana wakati wa kudai uhuru na hata baada ya taifa kuwa huru. Ilielezwa kuwa Bibi Titi aliunganishwa kwa Nyerere na dereva mmoja wa teksi ya nyumbani kwao mwaka 1954  na akawa mmoja wa waanzilishi wa chama cha Tanu.

Biti Titi alikamatwa na polisi Oktoba 1969 akiwa na waziri wa zamani wa kazi, Michael Kamaliza pamoja na maofisa wanne wa JWTZ na wote wakafunguliwa mashitaka ya kutaka kumuua na kumpindua Nyerere.

Ushahidi mwingi ulitolewa mahakamani na ilielezwa kuwa alikuwa akimwaga fedha ili kufanikisha mpango huo haramu kutokana na ufadhili wa mtu mmoja ambaye alikuwa nje ya nchi.
Je, nani alikuwa akimpa fedha? Utapata majibu haya katika toleo lijalo.
ITAENDELEA WIKI IJAYO

SOURCE: GLOBAL PUBLISHER