Wednesday 30 October 2013

UVCCM wampa Waziri Chiza siku 21


30th October 2013
Waziri wa Kilimo na Ushirika Christopher Chiza
Baraza Kuu la Umoja wa vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM) limemtaka Waziri wa Kilimo na Ushirika Christopher Chiza (pichani) kufanya uamuzi wa dharura wa kushughulikia matatizo ya wakulima wa korosho katika kipindi cha siku 21 na kutoa taarifa kwa umma hatua alizochukua.

Akizungumza jana na waandishi wa habari jana, Katibu Mkuu wa Umoja huo, Sixtus Mapunda, alisema baraza hilo limejadili kwa kina kuhusu matatizo yanayowakabili wakulima wa korosho ikiwa ni pamoja na kuyumba kwa bei ya korosho, malipo kuchelewa, tozo nyingi wanazolipishwa na udhaifu wa baadhi ya vyama vya ushirika.

“Baraza kuu limeamua kwa pamoja kuwa hali hiyo haivumiliki, na wananchi wana haki ya kulalamikia matatizo yanayoendelea katikan zao la korosho…Linamtaka Waziri Chiza sasa kushughulikia na hatua alizochukua na anazoendelea kuchukua ili kuwaokoa wakulima na unyonyaji mkubwa unaofanywa na walanguzi na wajanja wachache,”alisema Katibu huyo.

Alisema baraza hilo linasikitishwa na kasi ndogo ya utekelezaji wa agizo la kamati kuu ya CCM lililotolewa mwezi Mei mwaka huu liloitaka serikali kuwaita wadau wote na kuchukua hatua zitakazoleta ufumbuzi wa matatizo hayo kwa zao la korosho mapema iwezekanavyo.

Aidha alisema kuwa baraza hilo pia ilimejadili kwa kina juu ya uwepo wa tozo ya shilingi 1,000 kwa kila simu na kudai kuwa limebaini athari zitakazotokea katika utekelezaji huo.

Alizitaja athari hizo kuwa ni pamoja na ugumu wa ukusanyaji kutokana na hatua hiyo kupokelewa kwa hisia tofauti katika sekta ya mawasiliano hivyo suala hilo litazorotesha na kurudisha nyuma juhudi za kisekta.

Alisema kuwa athari nyingine ni idadi ya kuwa ya wateja kukosa huduma, kushuka kwa mapato na kuzorotesha uchumi kutokana  wateja kukosa mawasiliano na kuondolewa kwenye mitambo ya mawasiliano jambo litapelekea kukosa huduma na kushuka kwa mapato.

“Pia athari nyingine ni kukwamisha jitihada za kufikisha mawasiliano kwa wananchi wote…Ni dhahiri kuwa kuwepo kwa tozo ya 1,000 moja kwa moja kutadidimiza juhudi hizi kwani wawekezaji hawatapatiwa tena sababu ya kuwekeza vijijini pamoja na ruzuku wanayopata kupitia UCSAF,” alisema Mapunda

Alibainisha kuwa Baraza hilo limeitaka serikali kuachana na mipango isiyotekelezeka kwa kurejesha bungeni kwa hati ya dharura muswada wa marekebisho ya tozo hilo la simu ili kufanikisha malengo yake ya kufikisha mawasiliano ya simu kwa Watanzania kwa haraka alisema Katibu huyo.
 
CHANZO: NIPASHE