Thursday 31 October 2013

Babu Seya, watoto wake ‘watupa karata’ nyingine

“Katika hukumu yenu mlikubaliana na sisi kuwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu ilikosea kupokea ushahidi wa watoto , ila mlisema hiyo si hoja maadam kuna ushahidi unaounga mkono ushahidi huo ni bora,”PICHA|MAKTABA 
Na Tausi Ally, Mwananchi

Posted  Alhamisi,Oktoba31  2013  saa 24:0 AM
Kwa ufupi
Alidai kuwa ushahidi wa watoto hao ulichukuliwa bila ya kufuatwa kwa taratibu za uchukuaji wa ushahidi wa mtoto.

Dar es Salaam. Mwanamuziki Nguza Viking maarufu kama Babu Seya na wanawe kupitia Wakili Mabere Marando wameiomba Mahakama ya Rufaa, ifanye marejeo kuhusu hukumu iliyoitoa na ifute ushahidi uliowatia hatiani na adhabu ya kifungo cha maisha jela wanayoitumikia.
Marando aliliwasilisha ombi hilo, kwa takribani saa 2 mbele ya jopo la majaji watatu wa mahakama hiyo .
Jopo hilo linaongozwa na Jaji Nathalia Kimaro, akisaidiana na Jaji Mbarouk Mbarouk na Jaji Salum Massati.
Wakili huyo alisema wateja wake wanaoomba mahakama ifute ushahidi uliowatia hatiani washtakiwa na badala yake iwaachie huru.
Upande wa Mkurugenzi wa Mashtaka, uliwakilishwa na mawakili Jacksoni Mlaki, Angaza Mwaipopo, Emakulata Banzi, Joseph Pande na Apimack Mbarouk.
Hata hivyo mawakili hao waandamizi wa Serikali, waliyapinga maombi hayo kuhusu marejeo kwa madai kuwa yamepelekwa mahakamani bila usahihi.
Marando alidai kuwa mahakama iliteleza katika kutoa uamuzi uliowatia hatiani na kuwafunga maisha Babu Seya na watoto wake na kwamba kuteleza huko kunaonekana wazi wazi.
Alifafanua kuwa wakati wakifanya majumuisho ya kesi hiyo, mahakama ilijiridhirisha kuwa kulikuwa na makosa katika kupokea ushahidi wa watoto wanaodaiwa kufanyiwa vitendo hivyo.
Alidai kuwa ushahidi wa watoto hao ulichukuliwa bila ya kufuatwa kwa taratibu za uchukuaji wa ushahidi wa mtoto.
Alisema kwa msingi huo, ushahidi huo ulipaswa kufutwa.
“Katika hukumu yenu mlikubaliana na sisi kuwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu ilikosea kupokea ushahidi wa watoto , ila mlisema hiyo si hoja maadam kuna ushahidi unaounga mkono ushahidi huo ni bora,”alilalamika Marando.
Alieleza kuwa mtoto mdogo anapotoa ushahidi licha ya tahadhari, ana uwezo wa kutambua zuri na baya na kwamba lazima ushahidi wake uwekwe kwenye kumbukumbu ya maandishi na kwamba usipoonekana ushahidi wote ni batili na uondolewe.


Aliendelea kueleza kuwa kwenye hukumu wanayoilalamikia, anaiomba mahakama ijisikie kubadili uamuzi wa kuwafunga maisha wateja wake.
“Tuanaomba ushahidi wa wale watoto ufutwe, uondolewe mahakamani na washtakiwa waachiwe huru,”alisisitiza.
Upande wa mashtaka ulipaswa kuwaita mashahidi hao lakini nyie majaji katika hukumu yenu mlisema upande wa mashtaka uanahiari ya kumwita shahidi wanayemtaka wao.

SOURCE: MWANACHI