Saturday 28 September 2013

Nalaani Kufungiwa kwa Magazeti ya Mwananchi na Mtanzania; Serikali siyo “hausigeli” wa Taifa!



Kufungiwa kwa magazeti ya Mwananchi na Mtanzania kwa madai ya “uchochezi” ni mwendelezo wa matumizi ya sheria mbovu ya magazeti ambayo imekuwa ikitumika mara kwa mara kuzima au kuzuia mawazo na maoni ambayo serikali inayaoona kuwa hayafai. Kwa vile sheria hii imeweka madaraka makubwa kwa Waziri mwenye dhamana ya vyombo vya habari basi neno lake ni la mwisho na haitaji hata kufafanua maamuzi yake. Na baya zaidi ni kuwa uamuzi wake hauwezi kuhojiwa na mahakama yoyote.

Wakati umefika kwa vyombo vya habari, wananchi na wadau wengine kuanzisha vuguvugu litakalosababisha sheria hii ibadilishwe na hata kufutwa ili yeyote mwenye dhamana ya vyombo vya habari asichukue uamuzi bila kuangaliwa na chombo kingine (kama mahakama). Katika demokrasia ni muhimu kuhakikisha uwepo wa mfumo wa kusimamiana (checks and balances) ili kwamba mtu au chombo kimoja kisiwe na nguvu za kiimla (dictatorial powers). Kama Waziri angetakiwa kwenda mahakamani kufungua kesi dhidi ya magazeti haya – kesi ya uchochezi- ni wazi kuwa mahakama ingetakiwa kuangalia ushahidi uliopo na uzito wa ushahidi huo ukilinganishwa na haki za kikatiba zinazolinda vyombo vya habari na watoa maoni.'

Kwa msingi huo, japo ninatambua uwezo  na mamlaka ya Waziri kuchukua maamuzi aliyoyafanya nasimama kupinga na kulaani maamuzi haya kwani yanadumaza uhuru wa maoni, yanatisha vyombo vya habari na yanalengo la kuwalazimisha Watanzania kusoma na kusikiliza maoni yenye baraka za watawala tu na hivyo kuwapa watawala nguvu juu ya fikra na akili za wananchi. Lakini zaidi napinga uamuzi huu kwa sababu unaifanya serikali ni mlezi wa akili za wananchi kiasi kwamba kunaifanya serikali kuwa ‘hausigeli/hausiboy’ wa fikra za wananchi – kwamba wananchi hawajui kupima habari.
Ikumbukwe hadi leo hii hakuna kesi hata moja au mtu hata mmoja ambaye amewahi kushtakiwa na kukutwa na hatia ya kufanya jambo dhidi ya serikali au viongozi ati kwa vile amesoma habari ikamchochea kufanya jambo hili – maana ndio msingi wa hoja ya uchochezi! Napinga, Nakataa na ninakebehi madaraka haya ya Waziri.

Baada ya kusema hayo ni muhimu kusema pia kuwa uhuru wa habari na uhuru wa maoni unataka vyombo vya habari kuwajibika na kujiangalia vyenyewe (self-censorship) ili kuhakikisha kuwa habari wanazoandika zinaendana na ukweli na uhalisia na hili ni muhimu hasa kwa magazeti ambayo yanadai kuwa ni objective. Habari za kuvuta hisia (sensational news) zinatakiwa zibakie kwenye vyombo vya habari vya namna hiyo (tabloids). Kwa kadiri sheria hii bado ipo Wahariri na waandishi wajipime wasiwape sababu watawala kuingilia vyombo vyao vya habari.

SOURCE: MMM