Monday 16 September 2013

Msichana auawa kwa kupigwa risasi

15th September 2013
Msichana mmoja mjini hapa ameuawa kwa kupigwa risasi baada ya mtu mmoja aliyekuwa akiwinda kima kumkosa na kumpiga msichana huyo.


Tukio hilo limetokea juzi jioni katika kijiji cha Mashewa kata ya Kisiwani wilayani Muheza ambako marehemu huyo, Mwansiti Hamza (32) alipokuwa akiishi. Kaimu Kamanda wa polisi mkoa wa Tanga, Juma Ndaki, alisema kuwa Mwansiti alipigwa risasi na Victor Almasi (73), mkazi wa kijiji cha Misozwe wilayani hapa.

Kamanda Ndaki alisema mtuhumiwa huyo alitoka nyumbani kwake akiwa na bunduki saa 10 jioni kwenda kuwinda kima katika miti ya mikakao kwa ajili ya kuwapelekea mbwa wake kwa ajili ya chakula.

Ndaki alisema mtuhumiwa akiwa kwenye mawindo yake alimuona kima akiwa amekaa chini katika tawi la mti ndipo alipomlenga na bunduki.
Alisema kuwa baada ya kufyatua bunduki, risasi ilitoka na kwenda upande wa pili ambako msichana huyo alikuwa akichota maji na risasi hiyo ilimpiga tumboni na kumjeruhi katika mkono.  
CHANZO: NIPASHE JUMAPILI