Saturday 31 August 2013

Watanzania makuli wa dawa za kulevya- 2


                           
                              Dawa za kulevya zilizokamatwa hapa nchini siku za hivi karibuni 

Na Mwandishi Wetu, Mwananchi  (email the author)

Posted  Agosti31  2013  saa 7:30 AM
Kwa ufupi
Mbinu mbalimbali za kusafirisha dawa hizo hutumika ikiwemo kuwatumia watoto na wanawake kuficha katika rasta zao. sasa endelea


Uchunguzi wetu ulibaini kuwa unaweza kununua kinyago cha kimakonde na kukitoboa katikati kisha kuhifadhi cocaine, heroin au mandrax ndani kisha kukifunga vyema kama mzigo katika boksi na kuutuma katika nchi unayoitaka.
Hata hivyo, mbinu maarufu inayotumiwa na Watanzania wengi ni kumeza pakti za dawa za kulevya na kusafiri kwa njia ya basi hadi Afrika Kusini kisha kuvitoa kwa njia ya haja kubwa baada ya kufika.
Njia hii imekuwa na athari kiasi cha baadhi ya wasafirishaji kupoteza maisha; Mfano ni Watanzania wawili, Hassan Wanyama na Ali Mpili ambao walifariki mwaka jana kwa kumeza dawa hizo kisha kupasukia tumboni.
Mpili alifia katika nyumba ya wageni ya Braeside, Harare baada ya kukosa basi la moja kwa moja kwenda Afrika Kusini hivyo dawa hizo kupasukia tumboni.
Mpili alikuwa amemeza kete zaidi ya 80 za heroin.Watanzania wawili waliokuwa wakifanya mbinu za kuutorosha mwili wa Mpili nao walikamatwa.
Watanzania kukithiri katika biashara ya dawa za kulevya kumesababisha wengi hata wale waaminifu kuingia katika usumbufu mkubwa na kubatizwa majina chekwa yanayohusiana na dawa za kulevya.
“Mipakani siku hizi sisi Watanzania tunapekuliwa kivyetu, wakituona tu wanatuita ‘drugs’ tofauti na zamani tulijulikana kama taifa lenye watu watakatifu,” kinasema chanzo hicho.
Msemaji wa Tume ya Kudhibiti Dawa za Kulevya nchini (TDCC) Florence Mlay alizungumza na Mwananchi na kueleza kuwa, tume hiyo bado haina taarifa rasmi kuhusu ongezeko la watumiaji na wafanyabiashara wa dawa za kulevya Afrika Kusini.
“Kwa sasa hatuna ripoti yoyote kuhusu Watanzania Afrika Kusini, lakini kwa kuwa vyombo vya habari vinajitahidi kwa kasi basi tutalifanyia kazi hilo,” alisema Mlay.
Mipaka ya Tanzania
Tanzania kutumika kama moja ya njia kuu za kusafirisha mihadarati kunathibitishwa na tukio la Julai 2012 ambapo Mamlaka ya Mapato ya Afrika Kusini (SARS) ilikamata kiasi cha kilo 350 cha dawa haramu aina ya Mandrax zikitokea Tanzania, kisha zilipita Botswan na baadaye kuingia Afrika Kusini.
Julai mwaka huu, wanawake wawili wa Kitanzania Agnes Masogange na Melissa Edward walikamatwa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Oliver Tambo na mabegi sita yaliyosheheni dawa za kulevya aina ya methamphetamine maarufu kama `Tik’ yenye thamani ya Sh7 bilioni.

Msemaji wa SARS, Marika Muller alizungumza na Mwananchi na kueleza kuwa ‘hicho ni kiasi kikubwa cha dawa kukamatwa katika mpaka wowote wa Afrika Kusini’ kuwahi kutokea.
Mmoja wa watu wanaoishi Afrika Kusini, ambaye anafahamiana na Agness alisema kuwa, siku chache kabla ya kukamatwa kwake Uwanja wa Ndege wa Oliver Tambo, Masogange alionekana nchini Afrika Kusini akifanya ununuzi wa gharama kubwa katika maduka ya Johannesburg.
Kadhalika hata baada ya watuhumiwa hao kukamatwa Mwananchi lilibaini kuwa wamekuwa wakiwatuma baadhi ya watu kuwanunulia vipodozi na mahitaji mengine kwa ajili ya kuwapelekea mahabusu wanakoshikiliwa.
Ripoti ya UN
Ripoti ya mwaka 2013 kutoka Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Uhalifu na Dawa za Kulevya (UNODC) inaitaja Tanzania kuwa moja ya nchi kuu za Afrika zinazotumika kama njia ya kusafirisha dawa za kulevya.
Ripoti hiyo inaeleza kuwa Afrika Mashariki ikiwemo Kenya na Tanzania ni maeneo makuu yanayopitisha dawa za kulevya aina ya Heroin kutoka Afghanistan, Mandrax kutoka India na China na Cocaine kutoka Latin America.
UNODC inasema katika ripoti yake hiyo kuwa hivi sasa ni kawaida dawa za kulevya kusafirishwa kwa kutumia ndege za mizigo kutoka Afrika Kusini hadi Dar es Salaam au Zanzibar.
“Afrika Mashariki kwa sasa inawindwa zaidi na wasafirishaji wa dawa za kulevya kutoka Afghanistan na Pakistan kwa sababu ya udhaifu katika udhibiti wa bandari, fukwe, viwanja vya ndege na mipakani,” inasema ripoti hiyo.
Inaelezwa kuwa kingine kinachowavutia wafanyabiashara hao ni udhibiti dhaifu katika mamlaka za mapato na mfumo dhaifu wa kudhibiti uhalifu.
Kadhalika UNODC inaweka bayana ramani kuwa Heroin husafirishwa kutoka Afghanistan, kisha Pakistan na kuingizwa Tanzania, kabla ya kupelekwa Afrika Kusini.
Pia, ramani hiyo inaonyesha kuwa heroin na cocaine hupita zaidi katika mipaka ya Tunduma, Malawi na Musina, Limpopo. Pamoja na Afrika Kusini, kiasi kikubwa cha cocaine na heroin hupelekwa Marekani na Ulaya Magharibi.Ripoti hiyo pia inachambua kuwa, cocaine huzalishwa zaidi Latin America na kusafirishwa moja kwa moja hadi Tanzania, kisha Afrika Kusini.
Heroin nyingine hutoka Myanmar, kisha Thailand na huingizwa nchini kwa njia ya meli na mara chache kwa ndege. Dawa aina ya ethaloquone (mandrax) hutoka nchini India au China na kuja moja kwa moja nchini.

Kwa sasa maeneo mengine yanayotumika kupitisha dawa za kulevya nchini ni maeneo ya visiwani hasa Tanga na Zanzibar ambapo wasafirishaji hutumia boti binafsi ndogo. Mzigo unaposhushwa hapa hupelekwa kama mizigo midogo Dar es Salaam.

source: Mwananchi