Wednesday 28 August 2013

Usimamizi wa mitihani usiingizwe siasa


    Katibu Mtendaji wa Baraza la Mitihani Tanzania (Necta), Dk Joyce Ndalichako 



Posted  Jumanne,Agosti27  2013  saa 22:39 PM
Kwa ufupi
  • Pamoja na juhudi za Dk Ndalichako za kutoa ufafanuzi kuhusu ukweli wa suala hilo, hakuna aliyekuwa tayari kumpa sikio kutokana na suala hilo kupewa mtazamo wa kisiasa. Wananchi wengi, wakihamasishwa na wanasiasa waliishinikiza Serikali kutafuta chanzo cha hali hiyo.


Leo tumechapisha mahojiano maalumu kati ya gazeti hili na Katibu Mtendaji wa Baraza la Mitihani Tanzania (Necta), Dk Joyce Ndalichako kuhusu suala zima la usimamizi wa mitihani katika nchi yetu. Sote tutakubaliana kwamba suala la usimamizi wa mitihani limekuwa katika ndimi za wananchi wengi katika miezi ya hivi karibuni kutokana na matokeo mabaya ya mitihani ya kidato cha nne ya mwaka 2012 ambapo karibu nusu ya wanafunzi walifeli.
Kilichofuata baada ya kutokea kwa hali hiyo sasa ni sehemu ya historia, ingawa ni muhimu tukakumbushana tena kwamba hali hiyo iliibua sintofahamu katika Serikali na sekta nzima ya elimu. Bila kufanya tafakuri jadidi kuhusu sababu za wanafunzi hao kufeli mtihani huo, kila upande ulizungumza kivyake, huku Necta ikibebeshwa mzigo mkubwa wa lawama ambazo kusema kweli haikuzistahili. Moja ya lawama nzito ni kwamba kufeli huko kulitokana na Necta kubadili ghafla mfumo wa usahihishaji.
Pamoja na juhudi za Dk Ndalichako za kutoa ufafanuzi kuhusu ukweli wa suala hilo, hakuna aliyekuwa tayari kumpa sikio kutokana na suala hilo kupewa mtazamo wa kisiasa. Wananchi wengi, wakihamasishwa na wanasiasa waliishinikiza Serikali kutafuta chanzo cha hali hiyo. Hivyo, Serikali iliunda Tume ambayo ilipendekeza kufutwa kwa matokeo hayo na kuyasanifisha upya, uamuzi ambao ulionekana kwa wengi kuwa wa kisiasa. Hata hivyo, kiwango cha ufaulu baada ya kupitia upya matokeo hayo kilipanda kidogo, lakini hakikubadili picha halisi ya kwamba wanafunzi walioshindwa hawakuonewa na walistahili alama walizokuwa wamepewa awali na Necta.
Katika kupitia mahojiano yetu na Dk Ndalichako, wasomaji wetu watagundua kwamba kiongozi huyo bado anaona fahari kwa kazi iliyofanywa na inayoendelea kufanywa na Necta. Msimamo wake ambao nasi tunauunga mkono ni kwamba siYo tu siasa hazipaswi kupewa nafasi katika mchakato wa usimamizi wa mitihani, bali pia tusikubali kufikishwa mahali ambapo kila mwanafunzi atatakiwa afaulu mtihani hata kama hana sifa wala uwezo.
Tunakubaliana naye pia pale anapopinga dhana kwamba Necta inapaswa kushirikiana na wadau wote katika kazi zake. Jambo hilo haliingii akilini kwani kama alivyosema mwenyewe, taasisi yake ikifanya hivyo itafika wakati ambao wadau hao watataka washirikishwe katika kutunga mitihani inayotolewa na Necta. Lazima tukubali kwamba madhara ya kuingilia masuala ya mitihani ni makubwa mno na tukikubali wanasiasa waingilie mchakato wa mitihani tutakuwa tunaliangamiza taifa na kulipeleka kusiko.
Kwa kipimo chochote kile Necta imetoka mbali. Tukumbuke angalao kidogo Necta ilivyokuwa kabla ya kuteuliwa kwa Dk Ndalichako kuliongoza Baraza hilo mwaka 2005. Inaonekana wengi tumesahau kwamba kabla ya kuteuliwa kwake Necta ilikuwa ikisutwa na wananchi kwa kuendekeza vitendo vya kifisadi na rushwa.
Mitihani ilikuwa ikivuja kwa kiwango kikubwa na ilikuwa ikiuzwa kama njugu barabarani na kwenye taasisi mbalimbali. Baraza hilo halikuwa na uongozi wenye sifa za uadilifu na uchapakazi kama tunavyoshuhudia hivi sasa.
Sisi tuna matumaini makubwa katika uongozi wa Necta uliopo sasa. Chini ya uongozi huo, Necta sasa inaonekana kama mfano wa kuigwa na ‘Necta’ nyingine barani Afrika. Kama wasomaji wetu watakavyong’amua baada ya kusoma mahojiano yetu na DK Ndalichako, kiongozi huyo ana upeo, ubunifu na mwelekeo wa kuipeleka Necta kule inapopaswa kwenda iwapo ataungwa mkono.

source :Mwananchi