Tuesday 27 August 2013

Serikali yatakiwa kuibana saruji ya nje


Mkurugenzi Mtendaji wa Tanzania Portland Cement Company Limited (TPCC), Pascal Lesoinne (katikati) akizungumza na  wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Uchumi, Viwanda na Biashara walipotembelea kiwanda hicho kilichopo Wazo Hill  Dar es Salaam juzi.Na Mpiga Picha Wetu. 
Na Mwandishi wetu, Mwananchi  (email the author)

Posted  Jumatatu,Agosti26  2013  saa 10:49 AM
Kwa ufupi
Akizungumza na Kamati ya Bunge ya Uchumi, Viwanda na Biashara iliyotembelea kiwanda hicho mwishoni mwa wiki iliyopita, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya TPCC, Pascal Lesoinne,  alisema suala hilo kama halijapatiwa ufumbuzi litaathiri uhai wa kampuni nyingi nchini, hatimaye uchumi wa nchi.


Saruji kutoka nje inadaiwa kusababisha Serikali kupoteza mapato ya Sh25 bilioni kwa mwezi.
Dar es Salaam. Kampuni ya Uzalishaji Saruji Tanzania Portland Cement Company (TPCC), imeomba Serikali kuanzisha juhudi za makusudi zitakazosaidia kukabiliana na uingizaji bidhaa nchini zisizo na viwango ikiwamo saruji.
Akizungumza na Kamati ya Bunge ya Uchumi, Viwanda na Biashara iliyotembelea kiwanda hicho mwishoni mwa wiki iliyopita, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya TPCC, Pascal Lesoinne,  alisema suala hilo kama halijapatiwa ufumbuzi litaathiri uhai wa kampuni nyingi nchini, hatimaye uchumi wa nchi.
“Kampuni nyingi za Kitanzania za saruji hivi sasa zinakumbana na ushindani mkubwa kutoka kwa saruji itokayo nje hasa Pakistan,” alisema Lesoinne na kuongeza:
“Waingizaji saruji kutoka nje wanatumia ipasavyo mianya iliyopo kwenye mfumo wa forodha na uingiaji  bidhaa kwa kulipa kati ya asilimia tano mpaka 10,  hali ambayo inasababishia nchi hasara ya zaidi ya Sh25 bilioni.” 
Aliongeza kuwa Tanzania haihitaji saruji kutoka nje, kutokana na uwapo wa  viwanda vingi vinavyoweza fikia mahitaji ya nchi kikamilifu.
Pia, Lesoinne alisema kutokuwa na umeme wa uhakika, kumeongeza gharama za uendeshaji kwa kampuni yake na kwamba,  inatumia zaidi ya Dola 2 milioni za Marekani kwa mwezi kwa ajili ya umeme mbadala.
 Naye Mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila, alionyesha wasiwasi wake kuhusu jitihada zinazochukuliwa na mamlaka husika na kuzitaka kufanya uchunguzi sahihi kujua ukweli wa suala hilo.
“Hili ni suala nyeti. Kamati hatuwezi kulifumbia macho kwa sababu lina athari kwenye maendeleo ya uchumi wa nchini yetu,” alisema Kafulila.
Naye Mkurugenzi wa Viwanda Wizara ya Viwanda na Biashara, Eliness Sikazwe,   alisema Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk Abdallah Kigoda, tayari ameteua kamati ya wanachama saba kuchunguza suala hilo.
source: Mwananchi