Tuesday 27 August 2013

Mwekezaji aahidi usalama zaidi JNIA


 
Na Beatrice Moses  (email the author)

Posted  Jumatatu,Agosti26  2013  saa 22:21 PM
Kwa ufupi
  • Katika hatua nyingine mwekezaji huyo ametangaza kuwekeza ndege nane kwenye Shirika la Ndege la Tanzania(ATCL), mradi ambao unatarajiwa kugharimu dola za Marekani 100 milioni.


Dar es Salaam. Mwekezaji Sheikh Salim Abdullah ametangaza kuwekeza kwenye Uwanja Wa Ndege wa Kimataifa wa JK Nyerere Dar es Salaam (JNIA) kwa kufunga mashine za kisasa, ili kuimarisha usalama katika eneo hilo. Sheikh Abdullah ambaye ni Mwenyekiti wa Kampuni ya Maendeleo na Uwekezaji ya Al-Harathy ya Oman, alitangaza hatua yake hiyo jana, baada ya kutembelea maeneo mbalimbali ya uwanja huo, ambapo alisisitiza mashine zilizopo uwanjani hapo kwa sasa uwezo wake kiutendaji na kiusalama ni mdogo. “ Mashine hizi uwezo wake ni mdogo, dunia tunayoishi sasa imetawaliwa na magaidi uwanja wa ndege ni eneo muhimu ambalo linapaswa kulindwa kwa uhakika, mizigo inabidi kukaguliwa kwa umakini zaidi kwani wanaweza kuweka mabomu au vitu vingine vya hatari wakasababisha madhara makubwa alisema na kuongeza:
“Nimekuja kuwekeza hapa kwa kuitikia mwito wa Rais Jakaya Kikwete, amechoka sana inabidi sisi tumsaidie, ana nia nzuri ya kuhakikisha nchi hii inakuwa kiuchumi inabidi tumsaidie kuwekeza katika maeneo kama haya” alisema. Katika hatua nyingine mwekezaji huyo ametangaza kuwekeza ndege nane kwenye Shirika la Ndege la Tanzania(ATCL), mradi ambao unatarajiwa kugharimu dola za Marekani 100 milioni.
“ Tunanunua ndege nane ambapo nne ni aina ya Embraer ERJ-175 za Brazil na nyingine nne aina ya Mbombardier,kwa kuanzia tunapeleka vijana 10 wa kitanzania kwenda kusomea jinsi ya kuongoza ndege hizo” alisema.
Mkurugenzi Mtendaji wa ATCL, Kapteni Milton Lazaro, alieleza kuwa hatua hiyo ni faraja kubwa kwao na wana tumaini itatumiwa vyema kwa manufaa ya kukuza uchumi .
Kwa upande wake,, Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe alisema Serikali imefanya kazi kubwa kuvutia wawekezaji hao, ikiwa ni pamoja na kusafisha madeni yaliyokuwepo awali
 source: Mwananchi