Monday 26 August 2013

Mambo mbele kwa mbele



                             
                                                   Tido Mhando 


Posted  Agosti24  2013  saa 21:19 PM
Kwa ufupi
Tulifahamu kwamba alikuwa anapenda sana uchapaji wetu wa kazi, mimi na Masoud. Na hapana shaka, alikuwa mmoja wa wale ambao walichangia kuamua kwamba RTD iwakilishwe kwenye michezo hiyo ya New Zealand, maana alipenda sana michezo, hasa soka. Alikuwa “Yanga damu.”

Kwa zaidi ya miaka 40, Tido Mhando amekuwa akifanya kazi ya utangazaji. Kazi ya mapenzi yake maishani. Akianzia chini kabisa kama mtangazaji wa salamu hadi kufikia ngazi ya juu kabisa ya ukurugenzi mkuu. Kwa kipindi chote hiki amefanya kazi hii hapa Tanzania, Kenya na Uingereza. Kwa hiyo, anasimulia mengi aliyoyaona wakati wote huo kwenye makala zake hizi za kila Jumapili. Wiki jana, alihadithia vile mkurugenzi wa RTD siku hizo alipotangaza kwamba yeye Tido ameteuliwa kufuatana na timu ya wanamichezo wa Tanzania ambao walikuwa wakienda kushiriki kwenye michezo ya nchi za Jumuiya ya Madola (Commonwealth) huko New Zealand, mnamo Januari 1974. SASA ENDELEA...
Aliyekuwa mkurugenzi wetu hapo Radio Tanzania Dar es Salaam miaka hiyo, Paul Sozigwa, alitangaza uamuzi huo wa menejimenti kwenye mkutano wa watangazaji wote uliofanyika mwishoni mwa mwaka 1973.
Basi kwa kweli, niliuona mwaka huu kuwa kwa hakika, ulikuwa mwaka wangu. Kwa maana ndiyo mwaka ambao pia kwa mara ya kwanza, nilifanikiwa kusafiri nje ya Tanzania; yaani, baada tu ya kurejea kutoka Uganda, naambiwa tena natakiwa nipae anga za juu zaidi hadi Christchurch, New Zealand!
Kusema kweli nilifurahi kupindukia. Maana hata siku moja sikuwa na ndoto ya mapema hivi ya kwenda kule wengine wanakokuita mwisho kabisa wa dunia, bondeni kuliko bondeni kwenyewe. Uvuke Bahari ya Hindi hadi kwenye kisiwa hicho kilichopo kwenye Bahari ya Pacific.
Nilitoka kwenye mkutano huo nikiwa na tabasamu la kukata na shoka. Marafiki zangu wa karibu wakinitupia vijembe, wakinitania eti labda nimefanya kazi nzuri ya kufagilia makaburi ya mababu na bibi kule kijijini Kilulu, Mkuzi, Muheza, ndiyo maana mambo yananinyookea hivyo.
Nilicheka tu. Ama kwa kweli sikutarajia kwamba mkutano ule ungetokea kuwa kikao cha kihistoria hivi kwenye maisha yangu. Kikao cha mafanikio kwangu kuliko nilivyotarajia. Kikao kilichonifanya nifurahi kuliko maelezo.
Kitu kimoja kizuri siku zile pale RTD ni kwamba, mtu akifikwa na jambo zuri kama lile, kila mtu alikupongeza. Kulijengeka siku zile utamaduni mzuri wa kupeana hongera za dhati kwa mwenzenu aliyefanikiwa. Kwa hiyo, karibu wenzangu wote walinitakia kila la heri.
Tuliokuwa tumechaguliwa kwenda kwenye safari hii tulikuwa wawili, mimi na mwenzangu Abdul Omar Masoud Jawewa. Hakuwa rafiki yangu wa karibu hivyo, lakini tulielewana sana. Tulishirikiana na kushauriana kila ilipowezekana. Tulikuwa tunachangia kutayarisha kwa zamu kile kipindi maarufu cha saa mbili kasorobo, “Michezo”.
Masoud hakuwepo wakati mkurugenzi Sozigwa alipotangaza habari zile njema. Kwa hiyo, nikawa namsubiri kwa hamu afike ili nimpatie mchapo. Ulikuwa mchapo wa nguvu kwelikweli. Sikutaka apatiwe mchapo huo na mtu mwingine bali mimi mwenyewe; ili tuanze mara moja kupanga mambo mengine ambayo yangehusu safari yetu. Kwa sababu hiyo, wakati mwingi nikawa naangalia sehemu za langoni.
Lakini kwa kuwa bado nilikuwa nawajibika kuendelea na majukumu yangu mengine, nilijisahau na ghafla nikiwa niko maktaba ya sahani za santuri, nikamsikia Masoud anaulizia jamaa iwapo nimeonekana huko. Tayari alikuwa ameshapewa nyepesi nyepesi, akawa ananitafuta.
Tuliongea na Masoud kuhusu yapi ya kufanya haraka haraka, maana siku zilikuwa zimebakia chache, kama mwezi mmoja tu hivi na palikuwa na mambo mengi ya kufanya, ikiwa ni pamoja na kupata pasipoti za uhakika maana sote wawili tulikuwa hatuna, ukiacha ile ya muda tu ambayo mimi nilipewa kwa ajili ya safari ya Uganda.
Tuliamua kwenda wakati huo huo kumwona aliyekuwa Naibu Mkurugenzi na Mkuu wa Kitengo cha Habari na Matukio siku hizo, Sammy Mdee, ili tushauriane naye kuhusu safari yetu.

Sammy alikuwa mtu wa vitendo, mtu wa chapchap, aliyependa kuwasaidia na kuwashauri kwa karibu wale wote aliowaongoza. Alipenda mafanikio na matokeo mazuri. Na yeye, kama Paul Sozigwa, alikuwa mtu mwenye ushawishi mkubwa serikalini.
Tulifahamu kwamba alikuwa anapenda sana uchapaji wetu wa kazi, mimi na Masoud. Na hapana shaka, alikuwa mmoja wa wale ambao walichangia kuamua kwamba RTD iwakilishwe kwenye michezo hiyo ya New Zealand, maana alipenda sana michezo, hasa soka. Alikuwa “Yanga damu.”
Kwa hiyo, kama tulivyotarajia, Sammy alitusaidia sana. Alitupatia na barua ya kupeleka Idara ya Uhamiaji ili tupatiwe pasipoti haraka haraka, pamoja na maelezo mengine ambayo yangetusaidia kwenye matayarisho ya safari yetu. Tukaanza mara moja kuchakarika.
Lakini, wakati tukiwa mbioni hivyo, nami nilikuwa na jambo jingine binafsi ambalo nilikuwa nimepanga kulitekeleza aghalabu wakati huo huo. Nilikuwa nimeamua kuoa.
Kwa muda wa kutosha, nilikuwa tayari nimeanza kuona napata pata ile ari ya kufunga pingu za maisha. Kwa kuwa nilikuwa mtoto wa kwanza wa kiume kwenye familia yetu kubwa, niliona ni vyema nikachukua heshima yangu hii haraka iwezekanavyo.
Kwa ujumla, suala la kupata mwenza huyo halikuwa tatizo hivyo, ingawa hapana shaka umakini ulikuwa unahitajika, ingawaje kutokana na umaarufu niliokuwa nimejijengea tayari pamoja na utundu kiasi niliokuwa nao, sikuona kama kazi hii ingekuwa ngumu.
Labda ni pale mwanzoni tu nilipodhani kuwa ingekuwa vyema iwapo ningepata mwenza wa kutoka nyumbani kwetu Bonde. Hapa napo hapakuwa pagumu sana, ugumu ukatokea tu pale , kila ulipotaja jina la mmoja wao kwa wazee, uliambiwa huyo ni ndugu yako kwa hivi, huyu kwa vile na yule kwa lile. Ilimradi ikafikia mahali ambapo niliona kuwa labda jamaa wote wa Bonde ni ndugu zangu! Nikaamua kuachana na wazo hilo, sikutaka mambo ya kimila ya kuchinja mbuzi ama kondoo ili kuvunja undugu.
Kwa bahati, nilikuwa tayari kwa muda mrefu kiasi nimeshikana na binti mmoja wa mchanganyiko wa Kizaramo na Kinyakyusa. Nilikuwa nimemfahamu kiasi binti huyo tangu nikiwa bado Shule ya Sekondari ya Minaki, kule Kisarawe. Wakati huo yeye akisoma Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Jangwani, jijini Dar es Salaam.
Wakati huo, pale Minaki tulikuwa na utaratibu wa angalau mara moja kwa muhula, kuwa na “ball’, yaani tulikuwa tukiwaalika wanafunzi wa shule mojawapo ya wasichana ya jirani na kuwa “mapatina” wetu wa dansi. Hasa hasa, tulikuwa tumezoea kuwaalika hawa wasichana wa Jangwani.
Kwa ajili hii, uhusiano wetu na kina dada wa shule hii ulikuwa mkubwa sana, hata wakati mmoja mimi na marafiki zangu wa karibu pale shuleni, akina Sangwa Mwandu, Robert Mandawa, Victor Mnguto, Twaha Kizuguto, Robert Mwaimu na John Mhina, tulikuwa na kundi letu lililokuwa likifahamika kama “Bongo Boys”.
Mojawapo ya sifa ya Bongo Boys ilikuwa ni kucheza dansi na kwenye haya “maball”, tulikuwa tunashusha ngoma kali kweli kweli! Ghafla, kwenye mojawapo na sherehe hizi, tukaja kukutana na kundi jingine la wasichana wa hapo Jagwani ambao nao walikuwa wakali kama sisi, tukawataka urafiki na kuwapachika jina la “Bongo Girls”.
Kutokana na urafiki huu, tukawa mara kwa mara tunakwenda kuwatembelea dada zetu hawa pale shuleni pao. Tukatokea kuwa maarufu sana pale Jangwani. Ni wakati huu ndipo nilipomwona Mwangaza.

Yeye hakuwa miongoni mwa Bongo Girls, lakini alikuwa maarufu sana kwa kucheza mpira wa pete (netball). Ingawaje alikuwa mfupi, bado alikuwa na uwezo wa kuruka sana na kucheza vizuri mno mchezo huu, hata akafikia kiwango cha kuchaguliwa kwenye timu ya taifa.
Lakini cha zaidi, Mwangaza alikuwa na umbo la kupendeza mno, kiasi cha baadhi ya watu kumpa jina la utani la “Sunshine”. Sikuwahi kuwa karibu naye nilipokuwa Minaki, lakini mara baada ya kuanza kazi RTD, yeye akiwa bado Jangwani, tulikuja kukutana na kujenga urafiki mkubwa sana.
Haikuchukua muda, ikawa kwamba kila mtu aliyekuwa karibu nami alimfahamu Mwangaza na kwa muda wa miaka kadhaa, yeye na mimi tukawa karibu sana na ndiyo maana, mwishoni mwa mwaka huo wa 1973, nikawa nimepata hamasa ya kutaka kumuoa.
Mnamo mwanzoni tu mwa mwezi Desemba, nikafanya sherehe ndogo ya uchumba nyumbani kwao Tandika, nikiwa na baadhi ya marafiki zangu. Tuliamua tufunge ndoa Februari 1974, mara tu baada ya mimi kurejea kutoka New Zealand.
Wakati huohuo, mipango yetu ya safari, mimi na mwenzangu Masoud, ilikuwa ikiendelea vizuri. Tulifanikiwa kupata pasipoti haraka sana na mambo mengine yote yakawa yamenyooka. Lakini ghafla, siku moja ikaingia dosari.
Kama kawaida tulikwenda kwa pamoja kwa Sammy Mdee kupata maelekezo zaidi ya safari yetu hiyo. Sasa safari hii tulipofika, Sammy akatuambia kuna jambo alilokuwa anataka kutufahamisha.
Pamoja na majukumu mengine, mheshimiwa huyu ambaye alikuwa pia ni mjumbe wa Bodi ya Shirika la Ndege la Afrika Mashariki, East African Airways, alitueleza kuwa kwa muda amekuwa akijitahidi kuona iwapo katika kupunguza gharama za safari angeweza kupata tiketi moja ya bure ya ndege kwa ajili ya mmoja wetu, lakini kwa bahati mbaya haikuwezekana.
Tukiwa mimi na Masoud tumesimama pamoja huku tukiwa kimya sana, Sammy alituambia kwamba, baada ya kushindikana huko bado jitihada nyingine ziliendelea kufanyika ili kuona kama bado sote wawili tungeweza kwenda kwenye safari hiyo, lakini hilo nalo pia likawa limeshindikana kabisa.
Kwa hiyo, naibu huyo wa mkurugenzi akavuta pumzi na baada ya kunyamaza kwa muda, akatuambia ya kwamba kutokana na hali hiyo, wameamua ya kuwa aende mmoja wetu pekee na kutaja jina langu.
Lilikuwa ni pigo kubwa kwetu. Ulikuwa ni mstuko ambao hatukuutarajia hata kidogo. Ulikuwa ni uamuzi mgumu, lakini hatukuwa na la kufanya. Tuliondoka ofisini mle kwa Sammy Mdee kimyakimya.
INAENDELEA JUMAPILI IJAYO...

source: Mwananchi