Monday 29 July 2013

Wataka Katiba imwondolee Rais kinga kushtakiwa


Na Mussa Mwangoka, Mwananchi  (email the author)

Posted  Alhamisi,Julai25  2013  saa 12:58 PM
Kwa ufupi
Baadhi ya Wajumbe wa Baraza la Katiba Wilaya ya Kalambo mkoani Rukwa, wamesema wakati wakichangia maoni yao kwenye Rasimu ya Katiba hiyo iliyowasilishwa kwao na Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
 

Kalambo. Imependekezwa kuwa katiba ijayo itamke bayana kwamba Rais wa Jamhuri ya Muungano anaweza kushitakiwa baada ya kumaliza kipindi chake cha uongozi, iwapo atakuwa na tuhuma za kufanya makosa ya kikatiba katika utawala wake.
Baadhi ya Wajumbe wa Baraza la Katiba Wilaya ya Kalambo mkoani Rukwa, wamesema wakati wakichangia maoni yao kwenye Rasimu ya Katiba hiyo iliyowasilishwa kwao na Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
Mmoja wa wajumbe wa baraza hilo, Leonard Shalamwana alisema kuwa iwapo katiba itaeleza kwamba rais anaweza kushitakiwa baada ya kumaliza kipindi chake, itasaidia kuongoza taifa kwa kufuata misingi ya haki na uwajibikaji.
“Katiba ikiweka bayana kwamba rais anaweza kushitakiwa, itasaidia kudhibiti vitendo vya kifisadi, kujilimbikizia mali.......italeta uwajibikaji na kutakuwa na utawala wa haki unaozingatia sheria bila......tabia ya baadhi ya watu kujifanya wapo juu ya sheria itakoma” alisema William Kisabi mkazi wa Mtai.
Kisabi aliongeza kuwa viongozi wetu wamekuwa wakifanya ufisadi mkubwa ambapo hakuna hatua zozote zinazochukuliwa kwa kuwa katiba inawapa nguvu ya kutoshitakiwa mara baada ya kumaliza muda wake wa utawala kitu ambacho kinachangia kudumaza maendeleo ya taifa hili.
Faustine Mkula alipendekeza ibara ya 76 kifungu cha tatu kiondolewe ili kutoa fursa ya watu wengine wenye uwezo kugombea urais katika ya Serikali ya muungano na kuepesha tamaa ya watu kutaka kukaa madarakani kwa kipindi kirefu zaidi.
Ibara hiyo kifungu hicho inaeleza kwamba mtu aliyewahi kuwa Rais wa Tanzania bara au Zanzibar hatapoteza sifa ya kugombea nafasi za kugombea na kuchaguliwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano kwa sababu aliwahi kushika nafasi ya madaraka ya Rais wa Tanzania bara au Rais wa Zanzibar.
Pia wajumbe wa baraza hilo walipendekeza Rais kutoa taarifa ya hali ya hatari kwa bunge ndani wiki moja badala ya wiki mbili kama ilivyopendekezwa kwenye rasimu ya katiba ibara ya 80 kifungu cha kwanza hadi cha tatu.

CHANZO CHA HABARI HII: Mwananchi news paper