Wednesday 24 July 2013

Uhusiano wa Kenya na nchi za kigeni wazidi kuyumba


              Uhuru Kenyatta
Rais Uhuru Kenyatta (kulia) akiwa na Naibu Rais William Ruto baada ya kuwasili kutoka London, Uingereza Mei 9, 2013. Picha/PPS 
Na BENSON MATHEKA Na JUMA NAMLOLA
Imepakiwa - Monday, July 15  2013 at  09:24
Kwa Mukhtasari
Uhusiano wa Kenya na mataifa ya kigeni umewekwa katika darubini baada ya siku 100 za utawala wa Muungano wa Jubilee. Kipindi hicho, kumekuwepo mzozo kuhusu raia wa Nigeria Anthony Chinedu, Rais wa Amerika Barack Obama alikosa kuzuru na kesi za ICC bado zipo.

UHUSIANO wa Serikali na mataifa ya kigeni umewekwa katika darubini baada ya siku 100 za utawala wa Muungano wa Jubilee, hasa kufuatia kesi zinazowakabili Rais Uhuru Kenyatta na Naibu wake William Ruto katika Mahakama ya Kimataifa kuhusu Uhalifu, ICC.
Hivi majuzi, serikali ilipuuza hatua ya Rais Barack Obama wa Amerika ya kutozuru Kenya kwa sababu viongozi wake wanakabiliwa na kesi katika ICC alipotembelea mataifa matatu barani Afrika.
 
Naibu Rais William Ruto alisema kwamba hatua ya Rais Obama haikukosesha serikali usingizi kwa sababu Kenya ina marafiki wengi.
Kwenya hotuba yake ya kwanza kwa taifa baada ya kuapishwa, Rais Kenyatta alisema Kenya inathamini na kutegemea uhusiano wake na mataifa jirani ya Afrika Mashariki na bara la Afrika kwa jumla.
“Serikali yangu imejitolea kufanikisha biashara na  ushirikiano na mataifa ya eneo hili,” alisema Rais Kenyatta.
Alikiri kwamba Kenya itaendelea kushirikiana na mataifa ya Afrika chini ya Muungano wa Afrika kwa kuungana ili kupata suluhu la matatizo yanayoikuba bara hili.
Siku chache baada ya kuapishwa, alimtuma Naibu wake William Ruto kutembelea mataifa kadha barani katika kile kilichotajwa kama njia ya kutafuta kuungwa mkono dhidi ya kesi za ICC.
Kwenye hotuba yake alisema anaamini kwamba mataifa yote ya ulimwengu yanategemeana na kuahidi kukuza uhusiano na washirika wa kibiashara wa Kenya.
Alisema Kenya itaheshimu mikataba ya kimataifa  mradi tu iliwekwa kwa misingi ya heshima.
Majuzi uhusiano wa Kenya na ya mataifa kigeni uliwekwa kwenye mizani baada ya kuwatimua raia wa kigeni walioshukiwa kuhusika na ulanguzi wa dawa za kulevya maafisa pale ndege ya Kenya na maafisa walipozuiwa Nigeria kwa majuma mawili.
Serikali ilikanusha kwamba uhusiano wake na serikali ya Nigeria haukuathiriwa na tukio hilo huku ikilaumiwa kwa kukiuka kanuni za kimataifa ilipomtimua mfanyabiashara Antony Chinedu.
Baadhi ya Wakenya wanahisi kwamba Kenya inapasa kuimarisha sera za uhusiano wake na mataifa ya  kigeni ili kuvutia wawekezaji.
Wanasema huenda uchumi wa Kenya ukaathirika kwa sababu nchi za ulaya na Amerika zinajivuta kushirikiana na Kenya kutokana na kesi zinazowakabili viongozi katika ICC.
Kesi dhidi ya Bw Ruto imepangiwa kuanza Septemba 10 huku inayomkabili Rais Kenya ikitarajiwa kuanza Novemba mwaka huu.
Akihutubia wahariri na wanahabari katika ikulu ya Nairobi Ijumaa, Rais Kenyatta alisema Kenya iko tayari kushirikiana na taifa lolote linaloheshimu serikali kote ulimwenguni. Alisema kwa sasa uhusiano wa Kenya na mataifa yote ulimwenguni ni mzuri.
“Sijasikia ubalozi wa Kenya uliofungwa au nchi iliyofunga ubalozi wake nchini. Kwa hivyo ninaamini uhusiano wetu na mataifa ya kigeni ni mzuri,” akasema. Lakini inasubiriwa kuona  hatua atakazochukua siku zijazo baada ya  kuteua mabalozi.
Mashirika ya jamii kupitia Jukwa la Katiba, sasa yanaitaka serikali ikomeshe mtindo wa kutochukua hatua nchi inapotishwa na mataifa mengine ya Afrika.
Dharau
Rais wa mashirika hayo Bw Morris Odhiambo, alisema sera hii ya kunyamaza wakati raia wa kenya wanapohangaishwa unaifanya Kenya itazamwe kwa jicho la dharau nje ya mipaka yake.
“Katika kisa kama cha Chinedu, rais alipaswa kuchukua hatua kali na kuhakikisha anaikemea Nigeria. Lakini badala yake, serikali ilinyamaza na kuacha Wakenya kuwa mateka mikononi mwa mshukiwa huyo wa dawa za kulenya kwa wiki kadha. Huo ni uoga,” akasema.
Bw Odhiambo alisema ingawa Kenya inajifanya kuendeleza ushirikiano na mataifa mengine ya Afrika, haipaswi kuvumulia uchokozi wa aina yoyote. Alitoa mfano wa serikali ya Uganda kuendelea kukalia kisiwa cha Migingo na hata maafisa wake kuwapiga maafisa wa usalama wa Kenya waliotumwa kulinda mpaka wa kisiwa hicho.
“Hata wananchi wetu wanaposhambuliwa, hatusemi kitu. Lazima tuache uoga huu kama tunataka kuendelea mbele,” akasema.
Majuzi maafisa wa polisi wa Utawala wa Kenya walipigwa na kuumizwa na wenzao wa Uganda katika kisiwa cha Migingo baada ya ugomvi kuzuka kati yao.
“Huko nje tunadharauliwa sana. Rais na naibu wake wanapaswa kuwa na sera zitakazotupatia heshima. Wasidhani kuwa wanaangaliwa kwa njia nzuri eti kwa vile wao ni vijana,” akasema Bw Odhiambo.
Rais Kenyatta amesisitiza kuwa Kenya itashirikiana na mataifa ya Afrika zaidi kuliko mengine.

Source : Swahili hub