Wednesday 24 July 2013

NBC yawatoa hofu wananchi kuhusu akaunti ya Kiislamu


            
Baadhi ya wateja wa Benki ya NBC, wakifuturu katika hafla ya futari iliyoandaliwa na benki hiyo kwa wateja wake jijini Dar es Salaam, mwishoni mwa wiki. Picha na Joseph Zablon. 

Na Mwandishi Wetu, Mwananchi  (email the author)

Posted  Jumanne,Julai23  2013  saa 13:7 PM
Kwa ufupi
Akizungumza wakati wa hafla ya futari kwa wateja iliyoandaliwa na Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki, Naibu Waziri wa Fedha, Saada Mkuya Salum alisema bidhaa hiyo imeletwa katika muda mwafaka.


Dar es Salaam. Serikali imewatoa hofu Watanzania ikiwataka kutosita kujiunga na kutumia huduma za kifedha zinazofuata kanuni za Kiislamu kwa kuwa huduma hiyo ni mkombozi kwa wananchi wengi.
Akizungumza wakati wa hafla ya futari kwa wateja iliyoandaliwa na Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki, Naibu Waziri wa Fedha, Saada Mkuya Salum alisema bidhaa hiyo imeletwa katika muda mwafaka.
“Huduma hii hufuata sheria na kanuni za Kiislamu. Ni huduma inayojali na kufuata maadili na ni furaha kwa Serikali kuona kwamba hatimaye maadili sasa yanaingia hadi kwenye huduma za kifedha.
“Maadili yakiwa imara katika jamii, tunatarajia pia kupata uchumi imara wenye kukua na viwanda vyenye kuzalisha bidhaa na huduma zenye kukidhi mahitaji ya wote,” alisema.
Saada aliiomba NBC kuendelea kubuni na kuwaletea Watanzania huduma nyingine zenye kukidhi mahitaji mbalimbali ya wateja, wakubwa kwa wadogo, hususan mikopo kupitia Huduma ya Kibenki ya Kiislamu.
Aliitaka pia benki hiyo kutoa elimu kwa Watanzania ili waweze kufahamu kwa undani faida ya huduma hiyo ambayo iko wazi kwa yeyote bila kujali itikadi au imani yake ya kidini.
Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa NBC, Mizinga Melu alimuahidi Naibu Waziri kwamba benki hiyo haitaacha mipango yake ya kuisaidia Serikali kutekeleza kauli mbiu yake ya ‘maisha bora kwa kila Mtanzania’.
Naye Mkuu wa Kitengo cha Huduma ya Kibenki ya Kiislamu, Yassir Masoud alisema kuwa muda si mrefu NBC itaanzisha huduma za mikopo kupitia bidhaa hiyo, akisisitiza kwamba wanaelewa kuwa watu wengi wanaisubiri kwa hamu kubwa.
Huduma ya Islamic Banking ya Benki ya NBC ilizinduliwa Mei 2010.

chanzo: mwananchi news paper

cha