Tuesday 23 July 2013

Muundo wa Muungano: Tunatafuta Haki, Usawa au Ustawi?

July 22, 2013
By
                                    Union

Katika siku za karibuni baada ya kuzinduliwa kwa Rasimu ya Kwanza ya Katiba ya Tanzania, pamekuwepo na mjadala mkubwa kuhusu Muundo wa Muungano. Shauku kubwa imekuwa juu ya Muundo wa Serikali tatu. Waandishi, wachambuzi, wanasiasa na wasomi wametumia muda mwingi kutoa maoni yao juu ya muundo. Ukisoma kwa makini na kufuatilia mjadala huo,unapata hisia kuwa Muundo wa Muungano unachukuliwa kama mwarobaini wa matatizo ya muungano na umasikini wetu. Sehemu kubwa ya mjadala huo imejikita kwenye maudhui ya Haki na Usawa.
Sijakutana na msukumo wa kutosha kujadili kuhusu Ustawi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na watu wake, jambo linalonipa maswali ikiwa tuliungana ili tuwe SAWA, tugawane HAKI au TUSTAWI.  Ikiwa tutaweza kupata jibu la kwanini tuliungana, tutakuwa tumeshapata jawabu la Muundo unaofaa na sio kinyume chake. Lengo la andiko hili, ni kuongeza sauti kuwa lengo la Muungano wetu ni Ustawi, na kuwa, Muundo wa Serikali Mbili ndio njia ya kufikia ustawi huo, na kwamba changamoto za muungano (kero) sio suala la Muundo (structural) bali mfumo (systemic), na kuwa unaweza kufumua au kurekebisha mfumo bila kuathiri Muundo. 
Mantiki ya Muundo wa Serikali Mbili
Muundo wa Muungano wa Tanzania wa Serikali mbili haukutokana na nasibu bali mantiki na maridhiano yaliyotokana na tathmini za mazingira yaliokuwapo wakati huo. Mjadala mkubwa tokea Muungano kuanza na hata sasa umejikita kwenye idadi ya Serikali zinazofaa ambapo wako wanaozungumzia Serikali Moja, Serikali Mbili na Serikali Tatu. Aidha, mjadala huu kuhusu idadi ya Serikali haswa tatu na moja umekuwa ukifanyika kana kwamba ni wazo jipya au ugunduzi. Upo ushahidi kuwa hoja hii sio mpya na kuwa ilikuwa mezani wakati uamuzi wa Serikali mbili unafikiwa. Ushahidi huu unajidhihirisha kwa maneno ya Mwl. Nyerere ambaye ni mmoja wa Waasisi wa Muungano hapa chini:
“Tanganyika na Zanzibar zilipoamua kuungana na kuwa nchi moja, tungeweza kufuata mojawapo ya mifumo ya kawaida. Lakini tulishindwa kufanya hivyo kwa sababu ya udogo wa Zanzibar na ukubwa wa Tanganyika. Zanzibar ilikuwa na watu laki tatu (300,000) na Tanganyika watu milioni kumi na mbili (12,000,000). Muungano wa Serikali moja ungefanya ionekane kama Tanganyika imeimeza Zanzibar. Tulikuwa tunapigania uhuru na Umoja wa Afrika, hatukutaka tudhaniwe hata kwa makosa kwamba tunaanzisha ubeberu. Kwa hiyo mimi nilipinga mfumo wa Serikali moja. Shirikisho la Serikali Tatu lingekuwa ni gharama kubwa mno kwa Tanganyika. Zanzibar ingeendesha Serikali yake na kuchangia gharama za kuendesha Serikali ya Shirikisho; na Tanganyika ingefanya hivyo hivyo. Lakini ni dhahiri kwamba mchango wa Tanganyika ndio hasa ungeendesha Serikali ya shirikisho. Kwa hiyo, Tanganyika ingeendesha Serikali ya watu milioni 12 na pia ingetoa sehemu kubwa ya kuendesha Serikali ya Shirikisho la watu milioni12,300,000. Ni watu wanaofikiri kwa ndimi zao wanaodhani kuwa gharama ya Serikali yoyote kati ya hizi ingekuwa ndogo. Gharama ya Serikali ya Tanganyika isingekuwa ndogo, hata bila ya gharama za mambo yasiyo ya Shirikisho. Na gharama zote hizo kwa kweli zingebebwa na Tanganyika. Kwa hiyo ilitupasa tujiulize kwa nini tunataka kuibebesha Tanganyika gharama zote hizo; na hasa kwa nini tunataka Serikali ya Tanganyika? Hivi tuna hofu ya kwamba Tanganyika, bila kuwa na Serikali yake, itaonekana imemezwa na Zanzibar? Hofu yetu ni kwamba tukiwa na Serikali moja Tanganyika itaonekana kuwa imeimeza Zanzibar. Basi na tutafute mfumo ambao utaiondolea Zanzibar hofu hii ya kumezwa bila kuibebesha Tanganyika mzigo wa kuendesha Serikali mbili zenye uzito unaolingana. Hivyo ndivyo tulivyofanya, na hiyo ndio asili ya muundo wa Muungano wa serikali mbili. Badala ya kutungua mfumo uliopo kama wapumbavu, tulitazamia hali halisi yetu ilivyokuwa, na tukabuni mfumo uliotufaa zaidi” Mwl. J.K. Nyerere, Uongozi Wetu na Hatima ya Tanzania.

Nashawishika kuamini, hadi nitakapo shawishiwa vinginevyo kuwa mantiki iliyopelekea Serikali mbili ingali ina mashiko hata sasa, na kuwa kama mantiki haijabadilika, basi uhalali wa hoja yenyewe ya Serikali mbili nao haujabadilika. Kwa mujibu wa Sensa ya Taifa ya mwaka 2012, Idadi ya Watu katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni milioni 44,928,923, kati ya hao, Tanzania Bara ina idadi ya watu milioni 43,625,354 (tuchukulie wote walioko bara ni watanganyika) na idadi ya watu Zanzibar ni milioni 1,303,569 (tuchukulie hakuna Wazanzibari wanaoishi bara). Aidha, takwimu zinaendelea kueleza kuwa Tanzania bara ina kaya milioni 9,109,150 na Zanzibar ina kaya 253,608. Idadi ya ujazo wa Watu kwa Kilometa za Mraba (Population Density) kwa upande wa bara ni wastani wa watu 49 kwa kilometa moja ya mraba na Zanzibar ni watu 530 kwa kilometa moja ya mraba. Aidha, eneo la ukubwa wa ardhi ya Tanganyika na ardhi ya Zanzibar haujaongezeka tokea nchi hizi mbili zilipoungana mwaka 1964.
Kwa takwimu hizi, tujiulize, je kuna mabadiliko ya msingi katika idadi ya watu ambayo sasa hayatafanya Zanzibar kuonekana kumezwa na utaifa wake kupotea ikiwa tutakuwa na muundo wa Serikali moja? Je, baada ya miaka 49 ya Muungano, utaifa wa Mtanganyika umepotea na kupotea huko kunamaanisha kumezwa na uzanzibari? Je, watanganyika leo wamezanzibarishwa au watanganyika na wanzanzibari wametanzanianishwa zaidi? Na kama wametanzanianishwa zaidi, hii si ndio hatua katika kuelekea lengo la Umoja wa Afrika? Je, kasi ya ukuaji wa idadi ya watu Zanzibar (530 kwa kilometa ya mraba) wakati ukubwa wa eneo haujaongezeka hakufanyi umuhimu wa Muungano kuwa mkubwa zaidi leo kuliko 1964? Mwandishi mmoja wa nchi za Magharibi aliwahi kusema, “Unaweza kukataa kukubaliana na Mwl. Nyerere lakini ni vigumu kupinga mantiki yake”.
Hoja ya Usawa
Wanaopinga Muundo wa Serikali Mbili wanaibua hoja ya kutokuwepo kwa usawa kati ya Tanzania Bara na Zanzibar. Kinachostaajabisha ni kuwa kila upande unadai kuwa upande mmoja unafaidi zaidi ya mwingine. Wanaendelea kutuaminisha kuwa hata matatizo ya Muungano   (kero) yanatokana na Serikali mbili. Wako wanaosema kuwa Tanzania Bara inanufaika zaidi kushinda Zanzibar  katika Muundo uliopo kwa kuwa inaneemeka na kuendesha Serikali ya Muungano na hivyo kutumia rasilimali za Muungano kwenye kuendeleza Tanganyika kwa mambo ambayo sio ya Muungano. Hali kadhalika, wapo wanaosema kuwa Zanzibar inafaidi zaidi kwa kuwa ina Serikali yake, inajiamulia mambo yake na pia inafaidi yale ya Muungano kama kugawana misaada, kumiliki ardhi bara, kuongoza hata Wizara zisizo za muungano na mengineyo. Ili kuweka hali ya kile kinachodhaniwa ni usawa, inapendekezwa kuwa njia pekee ya kufikia usawa ni kuwepo kwa Serikali tatu.
Asili ya maumbile ya Tanganyika na Zanzibar, idadi ya watu katika nchi hizo mbili, na tofauti za ukubwa wa uchumi wa nchi hizo mbili hata kabla ya kuungana haviakisi Usawa. Ukweli huu mchungu unatueleza kuwa tunapojadili hoja ya Usawa hatuna budi kuzingatia  suala la Haki. Usawa peke yake hauwezi kutupatia jawabu. Tukiendeleza hoja ya usawa peke yake, wako watakaoupa usawa maana ya nusu kwa nusu. Mantiki ya usawa itatutaka tufike mahala serikali za Tanganyika na Zanzibar zichangie gharama za kuendesha Serikali ya Muungano ya watu milioni 44,928,923 nusu kwa nusu, na idadi ya wafanyakazi kwenye taasisi za Muungano iwe nusu kwa nusu. Hatua hii haitaleta msawazo na hakuna atakayefaidika zaidi ya Muungano kudhoofika. Swali la kujiuliza, tuliungana ili tugawane nusu kwa nusu? Hili ndilo lengo la Muungano?
Hoja ya Haki
Muundo wa Serikali mbili pamoja na changamoto zake umezingatia utoaji wa Haki. Kama alivyosema Mwalimu Nyerere, Muundo huo ulilenga kulinda Haki ya Zanzibar ambayo kimaumbile, ilitishiwa ikiwa tungekuwa na Muundo wa Serikali moja. Tanganyika  haikuwa na hofu hiyo ya kumezwa wakati ule na hata sasa. Ukweli wa hoja hii unajidhihirisha hata leo ambapo hata baada ya miaka 49 ya Muungano chini ya Muundo wa Serikali mbili, hofu ya Zanzibar kumezwa ingali ipo.  Napata tabu kuamini kuwa hofu hii itaisha kwa kuwa na Serikali tatu.  Somo tunalopata hapa ni kuwa mantiki ya Muundo wa Serikali mbili ilikuwa ni kutafuta urari kati ya USAWA na HAKI kati ya nchi mbili huru zililokuwa zikiungana. Je, tunaona uwezekano wa  Muundo wa Serikali moja au tatu kutibu jeraha la hofu ya ustawi wa Zanzibar?
Lengo la Muungano ni Ustawi
Pundamilia na Swala ni wanyama wa porini, wote hula majani na ni VITOWEO vya wanyama wanaokula nyama, sifa zote hizo zinawapa usawa. Hata hivyo, Pundamilia na Swala kwa maumbile yao wana utofauti, pundamilia ni mkubwa kuliko Swala, na hivyo Pundamilia HUITAJI MAJANI MENGI KULA ili ashibe tofauti na kiwango anachohitaji Swala. Lakini, Pundamilia na Swala wana hofu moja, HOFU YA KULIWA na wanyama wanaokula nyama kama Simba na Duma, hivyo ustawi wa kila mmoja, na ustawi wao kwa ujumla unategemea kushirikiana. Pundamilia ana macho makali na huona mbali lakini hana masikio makali, Swala ana masikio makali na husikia sana lakini haoni mbali. Pundamilia na Swala huamua kuendeleza ustawi wao kwa kula majani pamoja, bila kujali nani anakula majani kiasi kikubwa kuliko mwingine, kwa kuwa ustawi wao dhidi ya hatari ya kuliwa na wanyama wakali ni muhimu zaidi kuliko haki au usawa wa kila mmoja wao ukisimama peke yake.
Tatizo kubwa tunalokabiliana nalo leo ni kuwa busara iliyopelekea Muungano ni kubwa zaidi kuliko jumla ya baadhi ya busara ya wanasiasa na wananchi tulionao leo. Nguvu kubwa imeelekezwa kujadili Muundo kuliko lengo la kuungana. Muundo wa Muungano hauna budi utokane na lengo la kuungana na sio kinyume chake. Muungano wetu ni muungano wa watu, kabla ya kuungana watanganyika na wazanzibari walishachanganya damu na udongo, miaka 49 baadae, muingiliano ni mkubwa kuliko ilivyokuwa mwaka 1964.
Hatukuungana ili tuandike Katiba, tuliungana kurasimisha muingiliano wa damu uliokuwapo wa watu wa Tanganyika na Zanzibar. Hayo ma ‘print-out’ (Article of the Union) yanayotuzungusha kichwa leo sio lengo la Muungano bali ni matokeo. Tuliunganisha nguvu zetu kwa lengo la kulinda uhuru wa Tanganyika na mapinduzi ya Zanzibar dhidi ya wale wenye jicho la husuda nasi katika mazingira ya vita baridi vya dunia. Muungano wetu umeendelea kuwa wa kipekee na nchi pekee katika bara la Afrika ambayo imetokana na Muungano hadi sasa. Miaka 49 baadae, tishio la ustawi kwa nchi yetu katika mfumo wa utandawazi ni mkubwa na nchi zote duniani zinatafuta kuungana kama njia ya kukabiliana na utandawazi. Tishio la ustawi wa nchi yetu nje ya Muungano ni kubwa kwa Serikali ya Tanganyika na Serikali ya Zanzibar kuliko tukiwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Umoja unaoonyeshwa na baadhi ya watanganyika na ule unaoonyeshwa na baadhi ya wazanzibari katika kuunga mkono Serikali moja na tatu ni umoja dhaifu, umoja unaojengwa na chuki. Ni rahisi sana kuunganisha watu kwa chuki kuliko kuunganishwa na nia njema. Hata hivyo, chuki tangu kale na hata sasa haijawahi kuwa msingi endelevu wa kuunganisha watu. Matatizo ya Muungano wetu leo yanatokana na KUTOKUAMINIANA, HOFU na CHUKI za viongozi, na KUTOKUFAHAMIANA katika ngazi ya wananchi.
Nilifika mara ya kwanza Zanzibar mwaka 1994 nilipomaliza Darasa la Saba kwa kuwa Shule ya Msingi Forodhani ilikuwa na mahusiano na Shule Dada ya Msingi (Nimesahau jina) huko Zanzibar, tukatembezwa makumbusho ya Zanzibar na kuweza kuoanisha kile tulichojifunza kwenye historia darasani na tulichokikuta Zanzibar. Kuanzia hapo nimekuwa na marafiki wa kizanzibari na nimekuwa nikienda Zanzibar mara kwa mara kikazi na kibinafsi.  Kinyume chake, leo hii, mbara anaweza kusoma hadi akamaliza Chuo Kikuu hajawahi sio tu kufika Zanzibar, bali kuwa na rafiki Zanzibar, na vivyo hivyo kwa upande wa Zanzibar.  Kutokufahamiana huleta ombwe (vacuum) linalofidiwa na HISIA.  Kwa maoni yangu matatizo ya HISIA sio matatizo ya Muundo, na hayatatuliwi kwa KATIBA. Iwe Serikali moja au tatu, mafanikio ya Muungano yatatokana na KUAMINIAMA, KUHESHIMIANA na KUPENDANA.
Ni bahati mbaya kuwa wenye kuamini Serikali mbili, wamekuwa kimya wakidhani mantiki ya Serikali mbili inajieleza yenyewe tu katika kile kinachosemekana, “Chema chajiuza, Kibaya Chajitembeza”. Kwa kufanya hivyo, wametoa mwanya kwa wanaoupinga mfumo huo kwa sababu wanazozijua wao kuupaka matope na kupotosha mantiki yake. Mhe. Rais Ally Mohamed Shein wa Zanzibar aliwahi kusema, “Mtemewa mate na wengi hurowa”. Tumeacha Muundo uliopo pamoja na uzuri wake kutemewa mate kwa muda mrefu mwishowe umerowa.
Nampongeza Mheshimiwa Rais Kikwete kwa kuanzisha mfumo wa Serikali Mbili za Muungano na SMZ kukutana na kuzungumza chini ya Uenyekiti wa Makamu wa Rais. Tangu kuanzishwa kwa Mfumo huo, kero 13 zimeshajadiliwa, hoja 6 tayari zimepatiwa ufunguzi, hoja nyingine 3 ziko katika hatua ya mwisho kutatuliwa na hoja 4 zinaendelea kushughulikiwa. Toka mwaka 2012 hadi Aprili, 2013, vikao 9 vimekaa, vinne vikiwa vya Makatibu Wakuu na viwili vya Mawaziri. Aghalabu, hatua kubwa kama hii kujulikana kwa wananchi jambo ambalo linafanya watu kudhani kuwa Muundo ndio tatizo.
Umefika wakati wa Wananchi kuelimishwa kuhusu Muungano wetu, Muundo wake, faida zake na gharama za kuubadilisha muundo au kuvunja Muungano wenyewe. Kwa tulipofikia ni nadra sana jukumu hili kufanywa na wanasiasa wa pande zote maana sehemu kubwa ya wanasiasa hao ndio kero ya Muungano, kuliko kero zenyewe.
Na Mwandishi Wetu

Imenukuliwa kutoka :http://wewrite.or.tz/2013/07/mbadala-wa-muungano-kuelekea-katiba-mpya-fikra-za-nje-ya-boksi/