Wednesday 17 July 2013

‘Mazingira ya vyuo hayaruhusu ugunduzi’

      

 
Na Ibrahim Yamola, Mwananchi  (email the author)

Posted  Jumanne,Julai16  2013  saa 15:0 PM
Kwa ufupi

Waziri Mkuu Mizengo Pinda ni kati ya viongozi ambao kwa nyakati tofauti wamekuwa wakitoa kauli juu ya hali ya elimu nchini hususan kwenye nyanja ya sayansi na teknolojia.


Waziri Mkuu Mizengo Pinda ni kati ya viongozi ambao kwa nyakati tofauti wamekuwa wakitoa kauli juu ya hali elimu nchini hususan kwenye nyanja ya sayansi na teknolojia.
Mwaka 2008 akiwa Bungeni Mjini  Dodoma, alieleza kwa undani kuhusu masomo ya Sayansi na Hisabati akitoa tahadhari ya kukosa wanasayansi ambao ni watu muhimu katika maendeleo.
Katika maelezo yake, analinganisha ufaulu  wa masomo ya sayansi na sanaa katika shule za msingi na sekondari, ambako ilithibitika kwamba ufaulu wa masomo ya sayansi kwa kipindi cha kuanzia mwaka 2003 hadi 2007 ulikuwa umeshuka.
Akifafanua zaidi  anasema, mwaka 2001, katika mtihani wa kumaliza darasa la saba, asilimia 62 ya watahiniwa katika Wilaya ya Morogoro Vijijini walipata sifuri katika mtihani wa Hisabati.
Anaeleza kuwa katika mtihani wa kidato cha nne mwaka 2007, matokeo yanaonyesha kwamba asilimia 69 ya watahiniwa walishindwa mtihani wa Hisabati.
“Katika zama hizi za sayansi na teknolojia, hali kama hii inatisha na haiwezi kuruhusiwa kuendelea kutokea,” anasema Pinda.
Kutokana na hali hiyo, Serikali imekuwa ikifanya jitihada mbalimbali za kufungua milango kwa wadau ambao wanaweza kuchochea maendeleo ya sayansi nchini.
Moja ya njia hizo ni mkutano wa wadau wa sayanasi  ‘Smart Partnership Dialogue’ uliohusisha wadau kutoka kwenye mataifa mbalimbali ya Afrika, lengo likiwa ni kujadili jinsi bara hili litakavyoweza kutumia teknolijia kuchangia maenedeleo.
Mbali na mkutano huo ambao, wadau mbalimbali walishauri Serikali kuwekeza zaidi katika sekta ya elimu ikiwa ni pamoja na kutenga fedha za kutosha ili kuwezesha tafiti kufanyika katika vyuo na taasisi nyingine.
Mbali na mkutano huo, taasisi isiyo ya kiserikali inayojishughulisha na tafiti zenye mweelekeo wa kisera kwenye masuala ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu (STIPRO), inawakutanisha wadau  wa sekta ya elimu kujifunza jinsi ya utoaji wa elimu ya uvumbuzi katika elimu ya juu na vyuo vya ufundi nchini.
Mkurugenzi Mtendaji wa STIPRO, Dk Britrina Diyamett anasema, mazingira yaliyopo katika elimu ya juu na vyuo vya ufundi hayakidhi matakwa ya utoaji wa elimu ya uvumbuzi.
“Vyuo vyetu bado havina vifaa vya kujifunzia na kufundishia, walimu nao hawajaandaliwa kutoa elimu ya uvumbuzi, wanafundishwa kinadhalia kuliko vitendo. Tutafute vifaa vya kujifunzia ili mwanafunzi anapomaliza kufundishwa kwa nadhalia, ajifunze pia kwa vitendo.” Anasema Dk Diyamett

Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Aalbolrg Nchini Denmark, Profesa Palle Rasmussen anasema wanafunzi wanatakiwa kutambua umuhimu wa uvumbuzi na lengo la kukuza teknolojia.
Profesa Rasmussen anafafanua kuwa kunahitajika kutumia vitendo zaidi katika kufundisha na kuwashirikisha wadau wa sekta binafsi ili kuweza kufikia lengo la kuwa na wataalamu wa kutosha.
“Ili kuweza kutengeneza mfumo mzuri wa kuwapata wahitimu bora ni lazima kuwashirikisha wanafunzi na walimu wao katika utoaji na upokeaji wa mafunzo hayo ya uvumbuzi,” anasema Profesa Rasmussen.
Profesa Rasmussen anasema kuwa, taasisi za elimu zinaweza kuendesha tasinia ya uvumbuzi pasipo kutegemea serikali.
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dk Johnson Ishengoma anasema, haiwezekani kujenga vijana kuwa wavumbuzi wakati miundombinu ya kujifunzia bado haijaimarishwa.
Anaeleza kuwa Serikali inatakiwa kuwekeza fedha za kutosha katika vyuo  ili kuviwezesha kufanya tafiti zitakazosadia kuvumbua mambo mbalimbali yenye tija kwa taifa.
 “Itachukua muda mrefu kutoa elimu bora ya uvumbuzi kutokana na kutokuwapo kwa walimu wa kutosha wa kutoa mafunzo hayo,” anasema Dk Ishengoma.
Dk Isengamo anaeleza kuwa elimu hiyo ikitolewa ipaswavyo, mwanafunzi akihitimu mafunzo yake ya chuo hatasubiri kuajiriwa na badala yake atajiajiri mwenyewe.
Naye Vera Mugittu kutoka Muvek Development Solutions Ltd anasema, anasema ni vigumu kutengeneza mfumo huo kutokana na kutokuwepo kwa sera inayoratibu utoaji wa mafunzo hayo.
“Utoaji wa elimu ya uvumbuzi ni jambo gumu na la muda mrefu, serikali inatakiwa kutambua umuhimu wake na kuwekeza zaidi kwa kutenga fedha za kutosha,” anasema Vera.
Mhadhiri wa Kuchuo Kikuu Cha Dar es Salaam, kitengo cha  cha uhandisi na ueknolojia, Profesa Bavo Nyichomba anasema kukuwa kwa uvumbuzi kunategemea na ongezeko la wanafunzi wanaosoma masomo ya sayansi.
Anasema ubora wa uvumbuzi umekuwa hauna tija kutokana na viwanda vilivyokuwapo hapo awali kufungwa.
 “Ni jambo la aibu hadi vijiti vya meno na viwembe  tunategemea kutoka nje, vitu ambavyo kama viwanda vyetu vingeimarishwa na kujengewa uwezo tumepiga hatua katika uvumbuzi,” anasema Profesa Nyichomba na kuongeza:
“Tuanze kuboresha uvumbuzi kwa kuwarejesha wataalamu waliopo nje, waajiriwe na kutoa mafunzo sambamba na kutenga fedha za kutosha kuwezesha elimu ya juu na vyuo vya ufundi kutoa mafunzo kwa kiwango cha juu.”
Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk Shukuru Kawambwa anasema, jukumu la kutoa  elimu siyo la serikali pekee bali kila mwananchi ana mchango kwenye suala hilo.
 “Ili kutoa elimu iliyo bora ni jukumu la kila mmoja wetu, suala hili linahusisha nyanja mbalimbali. Kila mtu ana mchango katika kuhakikisha elimu yetu inakuwa bora. Walimu, wanafunzi na  wazazi kila mmoja akitekeleza wajibu wake ipasavyo tutafikia malengo,” anasema Dk Kawambwa.

chanzo: Mwananchi news paper