Tuesday 23 July 2013

Mahakama yaridhia Lwakatare kwenda India kwa matibabu

Mkurugenzi wa Usalama wa Chadema, Willifred Lwakatare akizungumza kuhusu hali ya ugonjwa wake akiwa katika Tasisi ya Tiba ya Mifupa Muhimbili (MOI) jijini Dar es Salaam jana.Picha na Fidelis Felix 

Na James Magai,Aziza Masoud  (email the author)

Posted  Jumatatu,Julai22  2013  saa 21:9 PM
Kwa ufupi
Alipata kibali hicho kwa kuwa anakabiliwa na kesi ya kula njama za kumdhuru Mhariri Mtendaji wa gazeti hili, Dennis Msacky


Dar es Salaam. Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam, imempa kibali Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Wilfred Lwakatare, akatibiwe nje ya nchi.
Lwakatare ambaye anasumbuliwa na maumivu ya shingo, kwa sasa amelazwa katika Taasisi ya Mifupa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (Moi) kwa uangalizi maalumu na kufanya mazoezi, alipata kibali hicho kwa kuwa anakabiliwa na kesi ya kula njama za kumdhuru Mhariri Mtendaji wa Gazeti la Mwananchi, Dennis Msacky.
Wakili wake, Nyaronyo Kicheere alililiambia gazeti hili nje ya mahakama kuwa Lwakatare anatarajiwa kupelekwa India, lakini akasema tarehe ya kusafirishwa inategemea na kukamilika kwa taratibu za hospitali alikolazwa, na kule anakopelekwa.
Mahakama hiyo ilitoa kibali ili akatibiwe nje ya nchi, baada ya Kicheere, kuiomba mahakama hiyo impe kibali ili akatibiwe nje kama ilivyopendekezwa na madaktari wake.
Akizungumza na gazeti hili, Lwakatare alisema ingawa yupo katika uangalizi maalumu, lakini amefikia uamuzi huo aliosema umekuja baada ya kujadiliana na madaktari wanaomuhudumia.
“Bado nafanya mazoezi, lakini kulingana na hali ilivyo imebidi nikae na madaktari nikashauriana nao nimewaomba niende nje ya nchi nikatibiwe kama itawezekana,”alisema Lwakatare.
Alisema pamoja na maombi hayo pia alikuwa anategemea kupata ruhusa kutoka mahakamani kwa sababu jana ilikuwa tarehe ya kuendelea kutajajwa kwa kesi yake baada ya kuachiwa kwa dhamana.
Alisema madaktari wanajaribu kufanya uchunguzi kwa kuzingatia uzoefu wao wao.
Awali aliwekwa katika Kitengo Maalumu cha Uangalizi wa madaktari na mazoezi kwa muda wa siku nne madaktari walimtaka kufanya mazoezi kwa saa tatu kwa siku ili aweze kupona tatizo hilo kabla kufikia hatua ya upasuaji.
Lwakatare ameomba kwenda kutibiwa nje ya nchi baada ya kukaa muda mrefu hospitalini hapo bila mabadiliko yoyote.
Lwakatare alifika Muhimbili Julai 10 kufuatia maumivu ya shingo ambayo chanzo ni chake ni ajali ambayo iliipata mwaka 2002.
Mbali na maombi ya kibali cha Lwakatare kwenda kutibiwa nje ya nchi, Wakili Nyaronyo pia aliiomba mahakama hiyo imchukulie hatua mshirika wa Lwakatare kwenye kesi hiyo Ludovick Joseph Rwezaura kwa kosa la kuandika makala kwenye mitandao ya kijamii, akilenga kujitetea dhidi ya shtaka linalomkabili na Lwakatare.

Wakili Nyaronyo alililalamikia kitendo cha Ludovick, akidai kuwa si sahihi kujitetea katika jukwaa lingine nje ya mahakama.
Katika mitandao hiyo Ludovick pamoja na kueleza uhusiano wake na watu mbalimbali akiwemo Naibu Katibu Mkuu wa CCM, Mwigulu Nchemba na Lwakatare, pia amekanusha tuhuma mbalimbali kuhusu kesi hiyo.

Source: Mwananchi news paper