Tuesday 23 July 2013

ICC sasa yaonya mauaji ya Darfur

Askari wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) wakiwa wamebeba jeneza moja kati ya saba ya miili ya askari wa Tanzania waliokuwa katika jeshi la kulinda amani la Umoja wa Mataifa (Unamid) baada ya kuwasili kwenye Uwanja wa Ndege wa Jeshi (Airwing) Dar es Salaam jana.Picha na Fidelis Felix 
Na Mwandishi Wetu, Mwananchi  (email the author)

Posted  Jumatatu,Julai22  2013  saa 9:31 AM
Kwa ufupi
Rais Jakaya Kikwete tayari amemtumia salamu Rais Omar al-Bashir kufanya uchunguzi na kuhakikisha wote waliohusika na mauaji hayo wanachukuliwa hatua kali.


Dar es Salaam na Mashirika. Wakati miili ya askari waliouawa Darfur ikiagwa leo kwenye Viwanj a vya Makao Makuu ya Jeshi, Upanga Dar es Salaam, Mwendesha Mashtaka wa Mahakama ya Kimataifa ya Jinai (ICC), Fatou Bensouda ametoa tamko kali dhidi ya mauaji hayo.
Katika taarifa yake aliyoitoa juzi, Bensouda alimwomba Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa(UN), Ban Ki-moon na wadau wengine wote ndani ya UN pamoja na Jumuiya za Kimataifa kufanya uchunguzi wa kina kuhusu tukio hilo na kuwachukulia hatua wale wote waliohusika.
Rais Jakaya Kikwete tayari amemtumia salamu Rais Omar al-Bashir kufanya uchunguzi na kuhakikisha wote waliohusika na mauaji hayo wanachukuliwa hatua kali.
Habari zilizopatikana   juzi zilidai kuwa askari hao wa kulinda amani waliuawa na kundi la wanamgambo wanaoungwa mkono na  Kundi la Janjaweed.
Waagwa leo
Wapiganaji hao saba wa Tanzania waliuawa walipokuwa wakilinda amani chini ya Umoja wa Mataifa na Afrika, Darfur, UNAMID.
Askari hao  wanaagwa leo kwenye Viwanja vya Makao Makuu ya Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) Upanga, Dar es Salaam.
Kaimu Msemaji wa JWTZ, Meja Joseph Masanja aliiambia Mwananchi jana kuwa Rais Jakaya Kikwete ambaye pia ni Amiri Jeshi Mkuu wa Tanzania, ni miongoni mwa mamia ya waombolezaji wanaotarajiwa kutoa heshima za mwisho kwa wapiganaji hao waliouawa Julai 13, kwenye mji, Darfur.

Source: Mwananchi news paper