Monday 22 July 2013

Ghana kuongeza umri wa kuolewa

18 Julai, 2013 - Saa 09:25 GMT

                                 
Mtakwimu Mkuu wa serikali ya Ghana, Bi Philomena Nyarko, amesema umri halali wa mwanamke kuolewa unapaswa kuongezwa kutoka miaka 18 hadi 23.
Bi. Nyarko amesema, hatua hiyo itawafanya wanawake kujiandaa vyema kiakili na kimwili kuzaa watoto, na kwamba, itapunguza ongezeko la idadi ya watu nchini Ghana kwa kati ya 15% hadi 20%.

Mapendekezo yake yamekuja wakati Wabunge nchini Nigeria wanajadili kuhusu kupunguza umri wa kuolewa kutoka miaka 18 ya sasa ili watu waweze kuoa na kuolewa katika umri mdogo zaidi.
Baadhi ya Wabunge Waislam, wametoa hoja kwamba, kuzuia watu kuolewa kabla ya miaka 18, unakiuka sheria za Kiislam ambazo zinaruhusu ndoa katika umri mdogo.
Nigeria ambayo inaongoza kwa idadi kubwa ya watu barani Afrika, imegawanyika kati ya Waislam na Wakristo.
Bi. Nyarko amesema kwamba, wanawake wanaochelewa kuolewa ama kuzaa hadi umri wa miaka 23 wanakuwa na afya njema.
“Inafahamika vizuri kwamba, matokeo ya afya njema kwa mama na mtoto, endapo atachelewa kuzaa hadi msichana anapokuwa amekomaa vya kutosha kwa ajili ya kuolewa na kubeba mimba ili kuokoa maisha ya mama na mtoto”, amesema Bi. Nyarko.
Watu wengi nchini Ghana ambayo ina watu takriban milioni 25.5 ni Wakristo.

Source: BBC Swahili