Tuesday 18 June 2013

‘Waislamu hawana uadui dhidi ya Wakristo’

Kwa ufupi  Kauli hiyo ilitolewa juzi na Mwenyekiti wa Baraza Kuu la Waislamu wa Tanzania (Bakwata) mkoani Mwan za, Sheikhe Salumu Bara.


Geita. Waumini wa madhehebu ya Kiislamu mkoani Geita, wametangaza kuwa hawana uhasama na waumini wa madhehebu ya Kikristo na kuthibitisha hilo, juzi walichangia harambee ya ujenzi wa Kanisa la African Inland Church, Dayosisi ya Kalangalala.
Waumini hao wa Kiislamu walichanga zaidi ya Sh1 milioni. Akizungumza katika harambee hiyo iliyoongozwa na Waziri Mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowasa, Katibu wa Bakwata wa Mkoa wa Mwanza, Sheikhe Salumu Bara, alisema Waislamu na Wakristo ni kitu kimoja.
Alisema ile imani iliyokuwa imejengeka katika jamii kuwa Waislamu na Wakristo ni maadui ni ya uwongo.
“Nisema Ukristu na Uislamu ni kitu kimoja, tumeamua kuishi kwa amani na upendo na sisi kama viongozi wa Bakwata Mwanza tumeanzisha umoja unaowashiriki watu 20 kutoka pande zote,” alisema Sheikhe Bara.
Kwa mujibu wa kiongozi huyo wa Kiislamu, umoja huo unalenga katika kueneza amani na kufuta udini ndani ya Mikoa ya Mwanza na Geita.
Alisema katika kuthibitisha kuwa Waislamu hawana chuki na Wakristo, wameamua kuchangia ujenzi wa kanisa hilo litakalotoa huduma za Mwenyezi Mungu.
“Hii inaonyesha kuwa Waislamu ni watu wa amani na si kama wanavyosema watu wengine,” alisema.
Katika hatua nyingine, viongozi hao wa Bakwata walitoa shukrani za dhati kwa Lowasa kwa kukemea udini na yeye binafsi kutokuwa na upendeleo wa kidini.